Jinamizi la mapinduzi ya wasimamizi laandama KTDA
KERO la mapinduzi ya mara kwa mara linalogubika uongozi wa bodi ya Halmashauri ya Majani Chai Nchini (KTDA) limejitokeza tena kufuatia kufurushwa kwa mwenyekiti Chege Kirundi.
Mwenyekiti hushikilia afisi kwa miaka mitatu, lakini katika kipindi cha miaka minne iliyopita, bodi hiyo imefanyiwa mageuzi mara nne – idadi kubwa zaidi katika siku za hivi majuzi.
Katika mabadiliko mapya, mwenyekiti wa bodi wa zamani, Enos Njeru amerejea katika kile kinachoashiria misukosuko ya uongozi kwenye bodi iliyotwikwa jukumu la kuongoza masuala ya wakulima 700,000 wa majani chai.
Aidha, naibu mwenyekiti James Ombasa Omweno aliondolewa na nafasi yake kutwaliwa na mhandisi Samson Mosonik Menjo, mkurugenzi katika kitengo cha tisa eneo la Bonde la Ufa Magharibi.
Mabadiliko hayo yalitangazwa na KTDA Machi 4 huku athari za hatua hiyo zikichipuka.
Bw Omweno alishikilia wadhifa huo kwa miezi mitano pekee baada ya kumrithi mtangulizi wake, Erick Chepkwony aliyezimia na kufa Nairobi mnamo Mei 21, 2026.
Migogoro ya ndani kwa ndani baina ya wakurugenzi wa halmashauri hiyo imejiri wakati viwanda vya majanichai vinakabiliwa na changamoto anuai ikiwemoi bei duni ya majanichai huku wakulima wakidai malipo bora.
Bw Njeru alisema baada ya kuchukua usukani timu yake itajitahidi kushughulikia masuala ya halmashauri hiyo kwa manufaa ya wakuzaji majanichai wanaomiliki mashamba madogo madogo katika sekta hiyo.
“Kuna mengi yanayohitajika kufanyika ili kubadilisha mkondo na tunahitaji usaidizi wote tunaoweza kupata kutoka kwa wadau na serikali kupanua soko la bidhaa zinazouzwa katika mataifa ya kigeni kwa mazao haya.
“Kuna mengi yanayohitajika kufanywa,” alisema Bw Njeru.