Habari

Jinsi Farouk na Itumbi walivyong’arisha Ruto chaguzi ndogo

Na Elvis Ondieki March 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HUKU dhana ya umma katika maeneo ya Mlima Kenya na Magharibi ikiashiria kwamba chama tawala cha UDA kinakabiliwa na shinikizo kuu, chaguzi ndogo zimesimulia hali tofauti kabisa kwa kutamba huku hali hiyo ikihusishwa pakubwa na wasaidizi wawili wa karibu na Rais William Ruto.

Duru ndani ya UDA zimehusisha pakubwa msururu wa ushindi uliofuatana kwenye chaguzi ndogo zilizofanyika Novemba 2025 na Februari 2026 na wasaidizi wa Rais Ruto: Farouk Kibet na Dennis Itumbi.

Bw Kibet na Bw Itumbi waliendesha kampeni za kichinichini kutoka kijiji hadi kingine kuhakikishia UDA ushindi.

Kwa mujibu wa duru za UDA, wasaidizi hawa wawili walishiriki mikakati kadhaa kabla ya wapigakura kuelekea debeni.

“Walipiga kambi vijijini kwa miezi miwili kabla ya uchaguzi mdogo Novemba,” zilisema duru kutoka chama hicho.

“Katika chaguzi ndogo Februari, walikuwa mashinani kwa karibu mwezi mmoja. Hizi hazikuwa siasa za kudhibitiwa kwa kibonyezo.”

Mikakati yao ilikuwa rahisi lakini iliyohitaji kujituma: kuunda mipangilio ya kampeni na viongozi wa maeneo husika, kujadiliana na wagombea hasimu, kuhudhuria mazishi na ibada za kanisa, kuvamia masoko, kubisha milango ya watu na kupeleka kipaza sauti katika kila fursa iliyopatikana.

Kibet aliangazia pakubwa Magharibi, akianzia uchaguzi mdogo wa Malava mwaka uliopita kabla ya kugeukia Wadi ya Kabras, Februari.

Akizungumza Kiluhya kwa ufasaha, alihutubia mikutano ya hadhara kwa lugha ya wenyeji na kujisawiri kama mtu anayefikiwa na kutangamana kwa urahisi nao.

Bw Itumbi, kwa upande mwingine, aliangazia Kaunti ya Embu na sehemu za Mlima Kenya Mashariki, zilizosheheni ushindani mkali kwa UDA.

Katika kinyang’anyiro cha Mbeere Kaskazini, Novemba 2025, wandani wa chama wanasema Bw Itumbi alichangia nafasi muhimu kusuluhisha ushindani wa uteuzi uliovutia wawaniaji chungunzima.

Wagombea saba waliashiria azma ya kupeperusha bendera. Taharuki ilitanda huku ikihofiwa uteuzi ulioshindaniwa vikali ungegawanya kura.

Kikao cha ngazi za juu kiliandaliwa Naivasha.

Waliohudhuriwa walijumuisha Gavana wa Embu Cecily Mbarire, Waziri Geoffrey Ruku na viongozi kadhaa wa kaunti.

Katika mkutano huo, Bw Itumbi aliwasilisha data ya kura ya maoni. Takwimu, duru zinasema, zilionyesha Leo Wamuthende alikuwa na nafasi bora ya kushinda.
Wagombea wakuu akiwemo Spika wa Kaunti ya Embu Justus Thiriku, Kinji Kwayo, Kariuki Mate, Dan Bongo, Stephen Makindu, aliyekuwa mbunge Njagagua na kaka yake Murage walikubali kujiondoa, na UDA ikanyakua kiti hicho.
Mbeere Kaskazini ilihusisha mikakati na majadiliano, chaguzi mbili za madiwani Februari katika maeneo ya Evurore na Muminji nazo zilihusisha uhamasishaji.
Kuanzia Januari kati hadi siku ya uchaguzi, Bw Itumbi alipiga kambi eneo hilo pasipo mapumziko.
Siku zake zilianza kabla ya jua kuchomoza na kuisha usiku wa manane. Alisafiri soko hadi jingine, akihutubia wauzaji. Katika mikutano hii ya ghafla wagombea walitangamana moja kwa moja na wapiga kura.