Jinsi Wakenya walivyosherehekea Krismasi Nairobi
MAELFU ya Wakenya walifurika katika vituo vya burudani katika Kaunti ya Nairobi Alhamisi kusherehekea Sikukuu ya Krismasi pamoja na sehemu nyinginezo duniani, kila mmoja kwa mtindo wake binafsi.

Huku wengi wakisafiri vijijini kujumuika na familia zao kwa sherehe hizo, matukio Alhamisi yalionyesha bayana idadi inayozidi kuongezeka ya Wakenya wanaochagua kukaa jijini kusherehekea.
Shughuli kati kati mwa jiji kuu la Nairobi (CBD) zilivutia huku wakazi wakijitokeza kwa wingi kupigwa picha na familia zao hali iliyowafaidi mno wapigapicha jijini waliokuwa tayari kupiga picha maridadi.

“Hii ndiyo siku pekee tunayotazamia. Biashara ilikuwa nzuri, naweza kwenda nyumbani na kitu kizuri leo na kununulia familia yangu kitu cha Krismasi,” alisema James Ochieng, mpiga picha CBD.
Bw Ochieng anasema kwa siku ya kawaida huwa anakusanya angalau Sh800 hadi Sh2, 500 kutegemea hali ya anga na idadi ya watu lakini Sikukuu ya Krismasi alienda nyumbani na Sh10,000.

Bustani ya Uhuru Park ilisheheni shughuli tele huku familia zikijitokeza kujiliwaza na kutazama maghorofa, barabara kuu ya Expressway, kupanda boti na kupigwa picha.
Hata hivyo sio wote waliokuwa Uhuru Park walikuwa na furaha. Wycliffe Aneda kutoka Vihiga aliyesema gharama ghali ya maisha imemwadhiri kihasi.

Katika majumba ya kibiashara ya Waterfront na The Hub, Karen, Wakenya walijivinjari kwa michezo anuai na kusakata ngoma.
Udadisi wa Taifa Leo ulifichua kwamba huduma ya kutuma vifurushi inayotolewa na kampuni maarufu za usafiri inatia fora huku magari yakiongezwa ili kukidhi idadi ya wateja wanaozidi kuongezeka.

Kulingana na Mkurugenzi wa Kampuni ya Ena Coach, Jervis Sundays, waliandikisha ongezeko la asilimia 50 katika biashara ya kutuma vifurushi.