Joho asisitiza ipo siku atakuwa rais wa Kenya
WAZIRI wa Madini na Uchumi wa Baharini, Bw Hassan Joho, amesisitiza hatalegeza kamba katika azma yake ya kuwa rais katika miaka ijayo.
Bw Joho aliwataka wakazi wa Pwani kujitenga na wanasiasa wanaotaka kuwatumia kupigana vita vya kibinafsi na badala yake watilie maanani umoja wa ukanda huo.
“Tusijikokote kupigana vita vya kisiasa vya watu wengine. Ipo siku jimbo la Pwani litazaa Rais wa taifa la Kenya. Siku moja watasikia Rais Hassan Joho, mimi nataka urais,” alisema Bw Joho, katika mazishi ya marehemu John Maitha.
Viongozi wengine waliohutubu walisisitiza kuhusu hitaji la umoja wa Pwani wakati siasa za 2027 zinapoendelea kupangwa pembe tofauti za nchi.
Mbunge wa Ganze, Bw Kenneth Kazungu, alisema miaka 20 baada ya kifo cha Bw Maitha ambaye aliunganisha Pwani nzima kwa ujumla, umoja wa viongozi hao umesalia ndoto.
“Saa hizi tunaona michakato ya siasa ikiendelea sehemu tofauti tofauti nchini, lakini sisi watu wa Pwani sisi bado tumekaa hatujui muelekeo wetu,” alisema Bw Kazungu.
Wakati huo huo, madiwani katika Kaunti ya Mombasa wameibua maswali kuhusu huduma duni za afya.
Wakati wa kikao cha kujadili makadirio ya bajeti kwa mwaka wa fedha wa 2025/2026, maafisa wakuu wa afya wakiongozwa na Afisa Mkuu wa Huduma za Kliniki, Dkt Shem Patta, na Afisa Mkuu Mtendaji wa Hospitali Kuu ya Rufaa ya Pwani, Dkt Iqbal Khandwalla, walilazimika kujibu maswali kuhusu utendakazi wa idara ya afya ya kaunti.
Katika kikao hicho cha mwishoni mwa wiki iliyopita, Diwani wa Chaani, Bw Frankline Makanga, alielezea wasiwasi mkubwa kuhusu jinsi taka za hospitali zinavyotupwa, akitaka maelezo ya kina kuhusu hatua za usalama na uwajibikaji.
Bw Makanga alilalamikia hali mbaya ya huduma za dharura katika Hospitali ya Port Reitz, hasa katika wodi za upasuaji na ajali, ambako alisema wagonjwa wameripotiwa kuachwa bila huduma zinazofaa.
Alitaja pia kucheleweshwa kwa ukarabati wa ukuta wa hospitali ya Chaani pamoja na paa linalovuja, jambo alilosema linaweka maisha ya wagonjwa na wahudumu hatarini.
Kwa upande wao, maafisa wa idara ya afya ya kaunti walijibu kuwa, miradi hiyo ni miongoni mwa inayopewa kipaumbele, lakini changamoto za kiufundi kama vile upimaji wa mipaka ndizo zinazochelewesha utekelezaji.
Diwani wa Wadi ya Mikindani, Bw Jacktone Madialo, alitaka ufafanuzi kuhusu kwa nini wadi za Mikindani na Miritini hazijajumuishwa kwenye mipango ya kustawisha huduma za afya.
Kulingana naye, Mikindani inastahili kujengewa zahanati au kliniki kwenye bajeti ya mwaka wa 2025/2026.
Aidha, alihimiza Kaunti kuimarisha kitengo cha mawasiliano ili kuzuia upotoshaji wa umma na kuwasiliana vyema na wakazi wa Mombasa.
Katika majibu yao, idara hiyo iliahidi kuwa ujenzi wa kituo cha afya cha Daraja la Nne katika eneo la Mikindani ni miongoni mwa masuala yanayopewa kipaumbele katika mwaka ujao wa kifedha.
Wakati wa majadiliano hayo, Mkurugenzi wa Wafanyakazi, Bw Suleiman Lugogo, aliwasilisha ombi la kuajiri wafanyakazi zaidi akieleza kuwa, uhaba wa wahudumu unawapa mzigo mkubwa wa kazi na kuwasababishia matatizo ya kiakili.
Mwenyekiti wa kamati hiyo, Bw Bernard Ogutu, aliwataka wakuu hao wa afya kuwasilisha maombi yao kwa maandishi ili kamati iweze kuyashughulikia kwa manufaa ya wakazi wa Mombasa.
Kikao hicho kilieleza haja ya kugawa rasilimali kwa usawa, kuwa na uwazi wa matumizi ya bajeti, na kuboresha mawasiliano na umma, huku Kaunti ikipanga masuala yanayolengwa kupewa kipaumbele katika sekta ya afya kwa mwaka wa 2025/2026.
Wakazi wa Mombasa wanatarajia kuona hatua madhubuti zikichukuliwa ili kuboresha huduma za afya, hasa katika hospitali za mashinani.