Juhudi za kumwondoa Kindiki, na kumrejesha Gachagua zaendelezwa kortini
WALALAMISHI wawili katika kesi ya kupinga kutimuliwa kwa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua wanapania kuwazuia majaji watatu kusikiza kesi hiyo huku wengine wakitaka Gachagua arejeshwe afisini.
Wawili hao wanawataka Majaji Eric Ogolla, Anthony Mrima na Freda Mugambi wajiondoe kusikiza kesi hiyo wakidai wanaendesha majukumu yao kwa mapendeleo.
Haya yanajiri huku kundi la walalamishi wengine watano wakishinikiza kurejeshwa afisini kwa Gachagua kwa misingi ya agizo lililotolewa Oktoba 18, 2024 na Mahakama Kuu ya Kerugoya iliyosimamisha kwa muda utekelezaji wa uamuzi wa Seneti wa kumwondoa afisini.
Uamuzi huyo pia ulizuia kuteuliwa kwa mtu mwingine kujaza nafasi ya Gachagua.
Alirejelea uamuzi wa hivi karibuni wa Mahakama ya Rufaa kwamba agizo la mahakama ya Kerugoya uliwekwa kando na jopo la majaji lililoteuliwa kinyume cha sheria, kundi hilo linasema hiyo inaashiria kuwa agizo hilo lingali hai na Bw Gachagua anafaa kurejeshwa afisini.
Ikiwa ombi hilo litakubalika, taifa litatumbukia kwenye utata wa kisheria wa uwepi wa manaibu wawili wa rais—Bw Rigathi Gachagua na aliyejaza nafasi yake Kithure Kindiki—hali ambayo waandishi wa Katiba ya sasa hawakutarajia ungejiri.
“Maana ya kisheria ya uamuzi wa Mahakama ya Rufaa ni kwamba hali ilivyokuwa kabla ya kutimuliwa kwa Gachagua idumishwe. Hii ina maana kuwa maagizo yalitolewa na Jaji Richard Mwongo katika mahakama ya Kerugoya yangali hali na yanapasa kuzingatiwa,” akasema wakili Stanleye Matiba kwenye stakabadhi alizowasilishwa kortini.
Kundi hilo la walalamishi linataka mahakama kuamua kesi hiyo na imrejeshi afisini Bw Gachagua.
Agizo lililositisha utekelezaji wa uamuzi wa Seneti wa kumfurusha Bw Gachagua lilikuwa limetolewa na Jaji Mwongo na ukabatilishwa na jopo la majaji watatu lililoteuliwa na Naibu Jaji Mkuu Philomena Mwilu, hatua iliyoharamishwa na Mahakama ya Rufaa.
“Mahakama ya Rufaa ilibatilisha hatua ya Naibu Jaji Mkuu kuteua jopo la majaji hao watatu wakiongozwa na Jaji Eric Ogolla. Hali hiyo sasa inaharamisha shughuli zote zilizofuatia ikiwemo kuondolewa kwa maagizo ya Jaji Mwongo na kuapishwa kwa Profesa Kindiki,” akaeleza wakili Matiba.
Hata hivyo, mawakili wa Gachagua wiki jana walielezea mahakama kwamba sasa hana haja na kurejeshwa afisini ila kubatilishwa kwa hatua ya kumwondoa afisini na kufidiwa.
Fidia hiyo ijumuisha malimbikizi ya mshahara wake na marupurupu ya muhula mzima wa miaka mitano.
Lakini watetezi wake Bw Gachagua— Bw Mathenge (Diwani wa wadi ya Baragwi katika kaunti ya Kirinyaga) pamoja na Peter Gichobi, Grace Muthoni, Clement Muchiri na Edwin Munene- wanaamini kuwa aumuzi wa kurejeshwa afisini au la kwa Bw Gachagua sio wake sasa.
Wanaamini kurejeshwa kwake unalenga kulinda uhalali wa maagizo ya mahakama na kudumishwa kwa utawala wa sheria.
“Hata baada ya Mahakama ya Rufaa kutoa agizo lake Profesa Kindiki bado anaendelea kutekeleza majukumu ya Afisi ya Naibu Rais kinyume na maagizo yaliyoko ya mahakama na licha ya kuharamishwa kwa mchakato uliofuatwa kumwezesha kuingia afisini,” akasema wakili Matiba.
Wakili huyo amewasilisha ombi mahakamani akitaka Profesa Kindiki azuiwe kutekeleza “Majukumu ya Naibu Rais wa Jamhuri ya Kenya” hadi kesi hiyo itakapoamuliwa.
Bw Matiba akaongeza: “Kwa kuendelea kushikilia afisi hiyo Profesa Kindiki anahujumu mamlaka ya Idara ya Mahakama na kukiuka Katiba hali inayofifisha imani ya umma kwa utawala wa kishera na heshima kwa taratiba za mahakama.
IMETAFSIRIWA NA CHARLES WASONGA