Kalonzo, Gachagua, Natembeya wajipa shughuli sherehe za Madaraka
VIONGOZI wa upinzani nchini Jumapili walisusia sherehe za Madaraka Dei huku wakikosa kuonekana kwenye hafla zozote za siku hiyo wakati ambapo Rais William Ruto aliongoza maadhimisho katika Kaunti ya Homa Bay.
Aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua akiwa ameandamana na wandani wake wa kisiasa walihudhuria ibada ya Jumapili katika kanisa la AIPCA Gatumbi, eneobunge la Lari Kaunti ya Kiambu.
Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka ambaye pia ni makamu wa rais wa zamani alituma tu risala za heri njema kwa Wakenya kupitia kurasa zake za mitandaoni.
Bw Musyoka hakuhudhuria hafla yoyote ya umma.
“Tunaposherehekea miaka 62 ya kujiongoza, lazima tujitahidi kujenga taifa ambalo limeungana, la amani na lenye ufanisi. Nchi yetu lazima iongozwe na imani ya uhuru, kujituma na ushirikiano ambao utafanya taifa letu liwe bora zaidi,” akaandika Bw Musyoka.
Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya na Naibu Gavana Philomena Kapkory walisusia sherehe za Madaraka huku wakiwakilishwa na Waziri wa Afya wa Kaunti Shem Ojwang’.
Gavana huyo wiki mbili zilizopita alinyakwa na kuzuiwa na makachero wa Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi Nchini (EACC) kutokana na tuhuduma za kushiriki ufisadi.
Alipigwa marufuku ya kutokanyaga makao makuu ya kaunti kwa siku 60 wakati ambapo uchunguzi kuhusu kesi ya ufisadi dhidi yake unaendelea.
Bw Natembeya kupitia vuguvugu lake la Tawe amekuwa mkosoaji mkubwa wa utawala wa Kenya Kwanza na baada ya kuachiliwa juzi, alishiriki misururu ya mikutano Magharibi mwa nchi akisema anaandamwa kwa sababu za kisiasa.