Kang’ata aenda likizo ya matibabu baada ya kuumia kisigino
GAVANA wa Murang’a Irungu Kang’ata ametangaza kwamba hatafaulu kuonekana hadharani kutekeleza majukumu yake kibinafsi baada ya kupata jeraha.
Kulingana na taarifa aliyoweka kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii, gavana huyo alikuwa akihudhuria mkutano wa kimataifa kuhusu Lishe Bora jijini Nairobi pale alipojikwaa na kupata jeraha kwenye mshipa wa kisigino.
SOMA CHAPISHO LA GAVANA HAPA
“Baada ya kufanyiwa ukaguzi wa matibabu, Gavana anaendelea kutibiwa na ameshauriwa kutofanya majukumu ya ofisini kwa mwezi mmoja ili kuruhusu apone kabisa,” ikasema taarifa hiyo.
Katika kipindi hicho, Naibu Gavana Stephen Munania ametangazwa kuwa atakayehudumu kwa niaba ya Bw Kang’ata, akisaidiwa na Waziri wa Fedha Profesa Kiarie.
Hata hivyo, watumiaji wa mitandao hawakuonekana kuridhika na tangazo la Bw Kang’ata kutoonekana hadharani kwa majukumu yake ya ugavana.
“Mwezi mzima Gavana hatakuwa kwa ofisi yake sababu ya kidole? Tuna mchezo sana katika taifa hili,” akasema Allano B.
“Tafadhali tutumie picha yako ukipokea matibabu katika hospitali ya Murang’a ili tuthibitishe kitu,” akachangia mtu mwingine aliyejiita Soar AboveMukiny.
Mchangiaji maoni mwingine akasema: “Hii ni mambo gani? Mwanamume anajikwaa kidogo halafu anajipa mapumziko kitandani ya mwezi mzima? Kunywa supu ya ngamia uende kazi. Na si unabebwa na gari, kwani unaenda kazini na miguu?”
Lakini kunao waliomtetea: “Kuwa mwanasiasa ni kazi ngumu. Kila jambo wanalofanya lazima lichambwe na wapambe kwenye mitandao.”