Kashfa Serikali kupeana paspoti kwa wageni wenye sifa tatanishi
MZOZO unatokota kufuatia madai kuwa pasipoti za Kenya zilitolewa kwa baadhi ya wageni wenye utata katika mazingira yanayotiliwa shaka.
Jana, vinara wa upinzani na aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga walitaka majibu kuhusu kashfa hiyo.
Wakati huohuo, wakili Wahinya Peter aliandikia Idara ya Uhamiaji akitaka apewe taarifa kuhusu wageni 28 anaodai wamepewa pasipoti za Kenya hivi karibuni, akitumia haki ya kupata habari chini ya Ibara ya 35 ya Katiba na Sheria ya Upatikanaji wa Habari.
Akizungumza mjini Nakuru, kiongozi wa Wiper Democratic Movement Kalonzo Musyoka alisema madai ya kutolewa kwa pasipoti kwa watu wanaoshukiwa kwa uhalifu wa kivita, akiwemo kiongozi wa wanamgambo wa Sudan, yanaweza kuweka Kenya katika mzozo wa kidiplomasia na kufanya raia wake kukaguliwa zaidi wanaposafiri nje ya nchi.
“Ni aibu kwamba serikali inatoa hati muhimu kwa wanamgambo. Hatuwezi kuruhusu Kenya kuwa maficho ya watu wanaotishia amani ya eneo hili,” alisema Musyoka.
Aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani katika utawala wa Uhuru Kenyatta, Fred Matiang’i, alihoji uadilifu wa mifumo ya uhakiki wa usalama akisema pasipoti ni stakabadhi muhimu ya kitaifa inayopaswa kutolewa baada ya uchunguzi wa kina.
Bw Maraga, ambaye sasa ni kiongozi wa United Green Movement, aliitaka serikali kufuta pasipoti inayodaiwa kutolewa kwa Algoney Hamdan Dagalo Musa, nduguye kamanda wa kikosi cha Sudan cha Rapid Support Forces (RSF), Mohamed Hamdan Dagalo maarufu kama Hemedti.
Algoney anaripotiwa kuwekewa vikwazo na Amerika na Jumuiya ya Ulaya. Kwa mujibu wa sheria za Kenya, mgeni lazima kwanza apate uraia wa Kenya baada ya kuishi nchini kihalali kwa angalau miaka saba mfululizo kabla ya kustahili kupewa pasipoti.