Maoni

MAONI: Kashfa za mafuta ni za wajuanao kwa vilemba wanavyovuana wakitofautiana

Na BENSON MATHEKA April 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KASHFA za mafuta nchini Kenya si geni; zinaanika jinsi sekta hii muhimu imetekwa na mitandao ya maslahi ya kibiashara, ushawishi na mianya katika udhibiti inayotumiwa na wenye nguvu.

Badala ya sekta hii kuwa mhimili wa kuimarisha uchumi na kupunguza gharama ya maisha kwa wananchi, imegeuka kuwa uwanja wa kunufaisha makundi maalum huku raia wakibaki kubeba mzigo wa bei ya juu.

Mfano wa wazi ni sakata ya Triton, ambayo ilifichua kwa mara ya kwanza ukubwa wa udhaifu katika usimamizi wa mafuta nchini.

Hasara iliyotokana na sakata hiyo inasemekana ilifikia zaidi ya Sh7 bilioni.

Hii iliweka wazi kuwa sekta hiyo haina tu mapungufu ya kiutendaji, bali pia imejaa ushawishi wa ndani uliowezesha ukiukaji wa taratibu.

Kesi imekuwa kortini kwa muda na nitakomea hapo kuihusu.

Miaka ilivyopita, badala ya kujifunza kutokana na makosa hayo, taifa lilijikuta tena likikumbwa na kashfa ya Sh19 bilioni iliyohusisha uagizaji na usimamizi wa mafuta, mara hii, ushindani ambao mfanyabiashara alidai shehena ya mafuta ya mabilioni ya pesa.

Hapa tena, maswali yalikuwa yale yale. Licha ya kelele nyingi za kisiasa na ahadi za kuchukua hatua kali, matokeo yake hayakuwa ya kuridhisha na haijulikani aliko mwanamke aliyedai kumiliki mafuta hayo.

Sasa, sakata ya hivi karibuni imesababisha maafisa wakuu kupoteza kazi kwa kisingizio kwamba walijiuzulu ikidhihirisha kuwa tatizo si watu binafsi bali ni mfumo mzima.

Ingawa hatua za kinidhamu zinaweza kuonekana kama suluhisho la haraka, mara nyingi huwa ni njia ya kupunguza shinikizo la umma bila kugusa mizizi ya tatizo.

Ukweli ni kwamba sekta ya mafuta imejengwa juu ya msingi wa maslahi, ambapo maamuzi mengi hayafanywi kwa kuzingatia ustawi wa wananchi bali faida ya makundi fulani.

Katika mazingira haya, taasisi za udhibiti zinakuwa dhaifu au zinashinikizwa, na mifumo ya uwazi inapoteza maana. Matokeo yake ni mzunguko usioisha wa kashfa.

Sioni kashfa hizi zikikoma na kuna sababu ya kuamini kuwa zinazolipuka ni chache tu pale wanaozithibiti wanapokosana.

Mafuta huzua migogoro ya kimataifa na mabilioni ya dola kutumiwa vitani kuyathibiti.

Hapa Kenya vita hivi ni vya wajuanao kwa vilemba wanazovuana mmoja akihisi kuchezwa shere.