Habari

Kauli mbiu ya ‘Wantam’ yaonekana kuwa chimbuko la masaibu ya Samidoh

Na CHARLES WASONGA June 10th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WIKI chache baada ya kukariri kauli mbiu ya upinzani ya “Wantam” kwenye mojawapo ya shoo zake, mwanamuzi Samuel Ndirangu Muchoki, almaaruf Samidoh, sasa anakabiliwa na hatari ya kukamatwa kwa kutelekeza majukumu yake kama afisa wa polisi.

Kauli mbiu ya “Wantam” imekuwa ikivumishwa na wanasiasa wa upinzani kuashiria kuwa Rais William Ruto hafai kupewa nafasi ya kuhudumu muhula wa pili 2027.

Samidoh, ambaye huimba kwa lugha ya Agikuyu, na ambaye ni afisa wa polisi wa utawala anayehudumu katika kitengo cha kupambana na wezi wa mifugo (ASTU), hajafika kazini tangu Mei 27, 2024 baada ya likizo yake kukamilika, mwajiri wake, Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) asema.

“Tangu wakati huo afisa huyo hajaonekana na haijulikani aliko,” inasema taarifa kutoka kwa NPS.

Majuzi, iliripotiwa kuwa Samidoh alihamishwa kutoka makao makuu ya polisi Ukanda wa Kati hadi kituo cha kikosi cha ASTU kilichoko Gilgil, kaunti ya Nakuru.

Lakini kulingana na taarifa ya polisi iliyotolewa Jumatatu, Juni 9, 2024 afisa huyo hajaripoti kazini kwa zaidi ya siku 10 “bila ruhusa au sababu maalum na kuchangia hatua za kinidhamu kuchukuliwa dhidi yake.”

Kulingana na Sheria ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi, Sura ya 84, ni hatia ya afisa wa polisi kutelekeza kazi.

Kwa hivyo, kwa mujibu wa sehemu ya 94 (1) “Afisa wa polisi anayekosa kufika kazini bila kuwa kwenye likizo au sababu maalum kwa zaidi ya siku 10, atachukuliwa kama ambaye ametelekeza kazi.”

Kulingana na sehemu ya 94 (3) “Afisa yeyote anayetelekeza kazi huwa ametenda kosa na anaweza kuadhibiwa kwa kufunguliwa mashtaka, kupigwa kalamu au kusukumwa jela kwa muda usiozidi miaka miwili.”

Maafisa wa polisi katika eneo la Gatumbiro, kaunti ya Nyandarua wameagizwa kumkamata Samidoh wakimwona.

“Aidha, agizo limetolewa kwamba NPS ikatize mshahara wake mara moja,” ikasema taarifa hiyo.

Mnamo Mei 16, Samidoh alivumisha kauli mbiu ya “wantam” katika mojawapo ya shoo zake, hatua iliyosifiwa na kukashifiwa kwa wakati mmoja mitandaoni.

Lakini siku chache baadaye mwanamuzi huyo alijitokeza pamoja na wanamuziki wengine wanaoimba kwa lugha ya Kikuyu, nyumbani kwa Naibu Rais Kithure Kindiki, na kubadili msimamo kwa kuunga mkono kampeni kumtaka Rais Ruto ahudumu kwa mihula miwili.