Kibagendi azimwa kufika majengo ya bunge
MBUNGE wa Kitutu Chache Kusini Anthony Kibagendi amezimwa kufika katika majengo ya bunge kwa muda usiojulikana, hadi atakapowasilisha barua ya kuomba msamaha, kwa kudai asasi ya bunge ‘imepigwa mnada’, imepoteza uhuru wake na kugeuka kuwa kikaragosi cha Serikali Kuu.
Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula alimkaripia Bw Kibagendi wakati wa kikao cha alasiri jana akitaja madai yake kama yanayoshusha hadhi na heshima ya bunge.
Ndani ya muda wa marufuku hiyo, Bw Kibagendi hataruhusiwa kutumia mali yoyote ya asasi ya Bunge ikiwemo afisi yake, ukumbi wa mazoezi na hataruhusiwa pia kuhudhuria vikao vya kamati.
“Sasa umesimamishwa kwa muda kufika katika Bunge kwa kuliharibia sifa hadi pale utakapowasilisha ombi la msamaha kupitia barua kwa Karani na barua sharti iwasilishwe katika bunge hili na ijadiliwe. Hili ni suala ambalo mawakili na majaji watalitaja kama dharau mbele ya mahakama. Nilimtazama Bw Kibagendi leo (jana) asubuhi akiongea kwenye runinga nikashtushwa na kile alichosema kulihusu Bunge hili,” Spika Wetang’ula akasema.
Akiongea wakati wa kipindi hicho cha majadiliano kuhusu masuala mbalimbali ya kitaifa katika Runinga ya Citizen, Bw Kibagendi alidai kuwa Bunge limenunuliwa.
Aidha, alidai kuwa Spika Wetang’ula na Naibu wake Gladys Boss “wameharibu” asasi hiyo kwa kukubalia idhibitiwe na Ikulu ya Rais.
“Kwa kudai kuwa Bunge hilo limenadiwa ilhali wewe ni mmoja wa wabunge, ina maana kuwa wewe pia ni bidhaa iliyonadiwa. Tunafaa kuwa waangalifu kuhusu yale tunayoyasema mbele ya kamera za vyombo vya habari au tunapohudhuria mijadala kwenye runinga,” Bw Wetang’ula akaonya.
“Ningependa kuwaambia kama Spika wenu kwamba hamna aliyeniita au kunipigia simu kunielekeza kuhusu majukumu yangu. Ikiwa kuna mtu anathubutu kufanya hivyo, nitampuuzilia mbali bila kujali hadhi yake,” akaeleza.
Bw Wetang’ula aliwataka wabunge, hasa wale wanaohudumu muhula wa kwanza, kujishughulisha na masuala yenye umuhimu kitaifa badala ya kutoa matamshi ya ‘kijinga’ katika maeneo ya umma.
“Ningependa kutoa wito kwa wazee katika Bunge hili kama vile James Nyikal (Seme), Aden Keynan (Eldas), Samuel Moroto (Kacheliba), T. J Kajwang (Ruaraka) na Mbunge wa Endebess Robert Pukose kuwashauri wabunge wachanga ili waweze kutoa kauli zenye manufaa ndani ya nje ya bunge hili,” akaongeza.
“Spika wa Bunge hili huwa hashiriki katika mijadala, huwa hapigi kura na haleti miswada na hoja. Wajibu wangu ni kuelekeza mijadala bila mapendeleo,” akaeleza Bw Wetang’ula.
Naibu Spika Bi Shollei alisema haikuwa sawa kwa Bw Kibagendi kutoa kauli za kumharibia sifa Spika Wetang’ula na yeye kama naibu wake ilhali hawakuwa katika kikao hicho ili wajitetee.