Kiini cha ajali mbaya iliyoua 16 usiku barabara ya Nyeri-Nyahururu chatambuliwa
MAUREEN Wambui alipoingia kwenye matatu Jumamosi jioni mjini Nyeri, alitarajia kufika nyumbani Mweiga, Kieni, mapema ili kuandalia binti yake wa miaka miwili Olivia Muthoni chakula cha jioni.
Kwa bahati mbaya maisha yao yalikatika pale matatu hiyo ilipogongana na lori lililobeba mbao karibu na Chuo Kikuu cha Teknolojia cha Dedan Kimathi (DeKUT) na kuwaua papo hapo.
Wambui na binti yake walikuwa miongoni mwa abiria 15 waliothibitishwa kufariki Jumamosi usiku.
Mtu mwingine alipoteza maisha hospitalini akipokea matibabu na idadi ya waliofariki ikawa 16.
Afisa wa Trafiki Kanda ya Kati, Elizabeth Vivi, alisema matatu hiyo ilikuwa na abiria 14 na watoto wawili, huku lori likiwa na dereva na makondakta wawili.
“Karibu na DeKUT, pikipiki ilitokea ghafla barabarani. Dereva wa lori alijaribu kuepuka kumgonga mwanabodaboda, kisha gari lililokuwa likielekea mjini Nyeri, likagongana na matatu,” alisema.
Watu wanne walinusurika, watu watatu wazima na mtoto mmoja na wakapelekwa hospitali na bado wako katika hali mahututi.
Walioshuhudia
Baadhi ya abiria wakikwama chini ya lori. Anthony Waweru, mmoja wa waokoaji wa kwanza, alisema lori lilikuwa likienda kwa mwendo kasi.
“Tulijaribu kuwaokoa kwa kuondoa mbao kutoka lori ili kupunguza uzito,” alisema Waweru, ambaye ni mwanabodaboda mjini Nyeri.
Vivi alisema hadi sasa, miili ya watu kumi imetambuliwa na sita bado hawajatambuliwa.
“Tunaomba familia zinazoweza kuwa zimepoteza wapendwa wao kujitokeza kusaidia kutambua miili,” alisema.
Familia zinazoomboleza zilipewa ushauri wa kisaikolojia katika mochari ya Hospitali ya Kaunti ya Nyeri.
Ajali hii ilitokea siku moja baada ya Mamlaka ya Uchukuzi na Usalama Barabarani (NTSA) kusitisha mfumo wake wa faini za papo hapo kufuatia agizo la mahakama.
Mkurugenzi Mkuu wa NTSA Nashon Kondiwa, alisema uchunguzi wa awali unaonyesha ajali ilitokana na mwendo wa kasi na uwezekano wa lori kutofaa kuwa barabarani.