Habari

Kilio ubomoaji ukiendelea katika soko la Gikomba

Na KEVIN CHERUIYOT April 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UBOMOAJI wa sehemu ya Soko la Gikomba Jumanne umewaacha maelfu ya wafanyabiashara wakiwa wamekwama na kukatiza riziki ambayo imehifadhi vizazi huku wengi wakiketi kwenye vifusi wakihofia kitakachofuata.

Soko la Gikomba linapatikana Pumwani, kaunti ndogo ya Kamukunji, umbali wa kilomita nne Mashariki mwa jiji kuu la Nairobi ni kituo kikuu cha uchumi.

Linafahamika kama soko wazi kubwa zaidi Afrika na linavutia zaidi ya watu 200,000 kila siku wanaojumuisha mtandao wa wafanyabiashara, wapakiaji, mawakala, wachuuzi wa chakula na wasafirishaji.

Kwa soko linalozalisha takriban milioni 80 kwa mwezi katika mapato ya kaunti kutokana na makato ya wauzaji pekee, lina umuhimu mkubwa.

Asili ya soko hili ni katika miaka ya 1950 lilipoanza kama kituo kisicho rasmi cha kibiashara karibu na Mto Nairobi.

Kadri miaka ilivyosonga, kiligeuka kuwa kituo kikuu kwa mavazi ya Mitumba kinachosambazia wauzaji kote nchini na hata nchi jirani.

Hata hivyo, huku ahadi za kujenga soko la kisasa zikishamiri, uhalisia wa sasa una uzito huku ukuaji wake ukiambatana na tafrani.

Kwa miaka mingi Gikomba imeandamwa na msongamano, miundomsingi duni ya majitaka na mioto inayozuka mara kwa mara inayoteketeza bidhaa za mamilioni uisku.

Wafanyabiashara walianza upya kutoka majifuni kwa hisia ya ukakamavu iliyogeuka sifa ya soko hilo.

Kando na masaibu hayo, kuna masuala ya kina: migogoro ya kila mara kuhusu ardhi, madai ya wamiliki wa kibinafsi na mitandao ya mabwenyenye wanaodhibiti maeneo ya soko hilo, hali iliyozua mazingira ya sintofahamu.

Visa vya moto vimehusishwa na migogoro hii na kuzidisha kutiliana shaka miongoni mwa wafanyabiashara.

Serikali imetangaza eneo hilo kuwa ardhi ya umma na kumaliza mivutano kuhusu umiliki ambayo imekuwepo kwa miaka mingi.

Uamuzi huo ulitoa nafasi kwa hatua ya majuzi, ubomoaji na maendeleo yaliyopangiwa.

Wafanyabiashara zaidi ya 6,300 hasa wanaojishughulisha na viatu wameathiriwa moja kwa moja na hatua ya Jumanne.

Wamehamishwa katika Uwanja wa Kamukunji ambao umetengwa kama eneo la muda.

Mwenyekiti wa Muungano wa Soko la Gikomba Kibathi Mbugua alieleza Taifa Leo kwamba mchakato huo umehusisha majadiliano.

Muungano huo kwa sasa una wanachama 100,000, kumaanisha wanachangia takriban Sh80 milioni kila mwezi kwa kaunti, hivyo kutekeleza wajibu muhimu katiuka uzalishaji wa mapato.

“Tulikubaliana na timu husika kuwa ni bora tushinikize mita 20 za ziada ili watu kwenye mita nyingine 30 na hizi mita 20 wapate nafasi katika soko litakalokuwa na ghorofa tatu. Tulishirikisha wauzaji na kukubaliana kuhusu mpango kwa hatua. Kwa karibu miezi sita, watarejea kwa Gikomba bora,” alisema Bw Mbugua.

Lakini mabadiliko hayajakuwa rahisi.