Habari

‘Kituo cha polisi’ chageuzwa kuwa baa

Na TITUS OMINDE May 31st, 2025 Kusoma ni dakika: 1

MIEZI mitatu iliyopita, mtu mmoja alizua mshangao nchini kwa kujaribu kuanzisha kituo cha polisi katika eneo la Kesses, Kaunti ya Uasin Gishu bila kufuata taratibu rasmi.

Collins Leitich, maarufu kama Chepkulei, 26, anayejulikana kama ‘Jenerali wa Ground,’ alifanya juhudi za kuanzisha “Kituo cha doria ya Polisi cha Cheboror” katika jengo alilokodisha eneo la Cheboror, bila kupata kibali kutoka idara zinazohusika na usalama.

Hatua hiyo ilizua gumzo mitandaoni na kufanya maafisa wa polisi wa kaunti ya Uasin Gishu kutembelea eneo hilo na kutangaza kwamba kituo hicho kipya kilikuwa haramu.

Ziara katika eneo hilo Alhamisi, miezi mitatu baadaye, ilibaini kuwa “kituo hicho cha polisi” kimegeuzwa kuwa baa. Rangi za polisi zimefunikwa kwa rangi nyeupe.

Philip Natui, mkazi wa Cheboror, alionyesha kuchanganyikiwa kuona jengo hilo likigeuzwa baa.

“Watu wa eneo hili walitarajia serikali ingechukua kituo hicho na kuweka maafisa wa polisi. Lakini tunashangaa kuona kimegeuzwa baa,” alisema kwa wasiwasi.

Aliongeza kuwa kugeuza kituo cha polisi kuwa baa kunahatarisha usalama katika eneo ambalo tayari lina changamoto kuhusu uhalifu.

Eunice Kirori, mfanyabiashara sokoni humo, alisema kuwa uamuzi huo si wa busara, akisema kuwa vijana wengi katika eneo hilo wameathiriwa na uraibu wa pombe.

“Umeharibu maisha ya vijana wengi. Kuwaacha waongezee matatizo kwa kubadilisha kituo cha polisi kuwa baa ni hatari,” alisema akihimiza serikali kuingilia kati.

Ingawa baadhi ya wakazi walishangilia juhudi za Leitich za kuanzisha kituo, wanasisitiza kuwa bado wanahitaji kituo halali cha polisi.

“Hili ni jengo la kukodisha na mwenye nyumba ana haki ya kulikodisha mtu yeyote anayetaka. Lakini sisi kama wakazi bado tunahitaji kituo cha polisi, si baa,” alisema mzee wa kijiji Isaac Maiyo.

Maiyo alibainisha kuwa mabadiliko hayo yalifanyika wiki mbili zilizopita na baa hiyo tayari inavutia wateja wengi.

Alitaka serikali isikie kilio cha wakazi kwani tayari kuna eneo lililotengwa sokoni kwa ujenzi wa kituo cha polisi.