Kocha wa soka, mkufunzi wa ndondi washtakiwa kuambia waandamanaji wavamie Ikulu
KOCHA wa zamani wa timu ya taifa ya soka, Harambee Stars, Robert Otiti, na mkufunzi wa ndondi katika ukumbi wa Muthurwa na Makongeni, Suleiman Bilali, Alhamisi walifikishwa katika Mahakama ya Milimani wakikabiliwa na mashtaka ya kuchochea waandamanaji kuvamia Ikulu ya Nairobi wakati wa maandamano ya Jumatano, Juni 25, 2025.
Afisa anayechunguza kesi hiyo aliomba mahakama iwazuilie washukiwa hao kwa siku 10 ili kutoa muda wa kukamilisha uchunguzi.
Hakimu Mkuu Mwandamizi wa Mahakama ya Milimani, Bi Dolphina Alego, alielezwa kuwa washukiwa hao wawili walituma ujumbe mnamo Juni 24, 2025, uliosambazwa kwa kasi kwenye mitandao ya kijamii wakiwataka wananchi wakutane jijini Nairobi kwa lengo la kuandamana na kuelekea Ikulu.
Bi Alego aliambiwa kuwa polisi waliweza kufuatilia ujumbe huo na kubaini kuwa ulitolewa kupitia jukwaa la X Space la mitandao ya kijamii, na kwamba nia yake ilikuwa kuchochea ghasia na kuvunja sheria kwa kiwango kikubwa.
“Polisi wanahitaji muda wa kuchunguza simu za washukiwa kwa kutumia teknolojia ya kisasa na pia kuchukua taarifa kutoka kwa mashahidi wanaokusudiwa,” alieleza afisa huyo wa uchunguzi akiomba mahakama kuwapa siku 10 wakamilishe uchunguzi.
Hata hivyo, mawakili wa utetezi, Abner Mango na Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino, walipinga ombi hilo wakisema haki za washukiwa hao zilikiukwa.
Bw Mango alisema kuwa Otiti na Bilali ni raia maarufu walioiletea nchi heshima kupitia sekta ya michezo.
“Otiti ni kocha wa zamani wa Harambee Stars aliyewahi kuiongoza timu hiyo kuifunga Somalia mabao 14 kwa bila, naye Bilali ni mkufunzi maarufu wa ndondi,” alisema Mango.
Mahakama itatoa uamuzi kuhusu ombi hilo Ijumaa.