Habari

Kongamano la uchumi wa baharini laanza Ufaransa Macron akiisuta Amerika

Na PAULINE ONGAJI June 9th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

NICE, UFARANSA, Juni 9, 2025

MAKALA ya tatu ya Kongamano la Umoja wa Mataifa kuhusu masuala ya baharini limeng’oa nanga jijini Nice, Ufaransa, huku Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron akiikosoa Amerika wazi wazi kwa kukatiza ufadhili wake katika masuala ya mazingira.

Akizungumza katika hafla na wanasayansi iliyoandaliwa Jumapili Juni 8 usiku, Rais Macron alisema kwamba hatua hiyo inatishia kuathiri uwezo wa ulimwengu kukabiliana na janga la kimazingira, hasa wakati huu ambapo kumekuwa na ongezeko la majanga yanayotokana na ongezeko la joto baharini.

“Sayansi ya kimataifa bado inategemea pakubwa ufadhili wa Amerika,” alisema.

“Lakini inahuzunisha kwamba tunaishi wakati huu ambapo ufadhili huu unaondolewa. Ni wakati wa kufikia uamuzi kuhusu ulimwengu wote kwa jumla.”

Amerika ambayo haijahudhuria kongamano la mwaka huu, imekashifiwa kwa kulegeza jitihada zake katika masula ya kimazingira ulimwenguni hasa katika kipindi cha hivi majuzi.

Rais Macron aidha alitangaza kwamba takriban marais na wakuu wa serikali 30 wamekubaliana kuunga mkono marufuku ya muda dhidi ya uchimbaji madini na matumizi ya rasilimali za baharini kupindukia.

Zaidi ya viongozi 50 wakuu duniani wanatarajiwa kuhudhuria kongamano hili ambalo litatia nanga mwishoni mwa wiki. Shabaha kuu itakuwa kutia saini Mkataba wa makubaliano wa High Seas Treaty, makubaliana ya kimataifa yanayonuiwa kuhifadhi mazingira na biodiversity katika maeneo mbali na hiamya yake.

Kwa Kenya, inayojivunia ufuo wa ukubwa wa zaidi ya kilomita 600 na sekta ya uchumi wa baharini ambayo imeendelea kukua, maamuzi yatakayofikiwa kwenye kongamano hili yana uzito mkubwa.

“Jamii zinazoishi kwenye ufuo katika kaunti kama vile Mombasa, Kilifi, na Lamu tayari zinaendelea kukumbwa na changamoto ya kuongezeka kwa viwango vya maji ya bahari, kupungua kwa samaki na uchafuzi wa mazingira wa plastiki,”alisema Kevin Lunzalu, mwanaekolojia katika shirika la African Wild Life Society.

Baadhi ya wajumbe wakiingia katika Sehemu ya maonyesho ya mashirika yanayohusiana na rasilimali za baharini katika kongamano la Umoja wa Mataifa kuhusiana na uchumi wa baharini jijini Nice, Ufaransa. Picha|Pauline Ongaji

Kwa upande mwingine, Kenya imekuwa mstari wa mbele katika masuala ya uhifadhi wa bahari. Mwaka wa 2018, kongamano la kwanza kuhusu uchumi endelevu wa baharini lilifanyika jijini Nairobi, na katika miaka ya hivi majuzi, serikali imeonyesha nia ya kupunguaza uchafuzi wa mazingira kwa plastiki na kuimarisha maeneo ya baharini yaliyolindwa.

Hata hivyo, washikadau na wanaharakati wa ufadhili wa kimazingira wanaonya kwamba pasipo ushirikiano na ufadhili katika ngazi za kimataifa, jitihada hizi zitagonga mwamba.

Katika mahojiano na afisa mmoja katika wizara ya uchumi wa baharini na uvuvi, alisema kwamba tayari sekta hiyo humu nchini inakumbwa na changamoto mbali mbali, ikiwa nii pamoja na uhaba wa fedha.

“Hii inamaanisha kwamba kukatizwa kwa ufadhili na Amerika kunatia wasiwasi,” alisema Bw Lunzalu.

“Shughuli zetu nyingi za ufadhili na utafiti zinatokana na ufadhili wa kimataifa, kumaanisha kwamba kupungua kwa ufadhili huu kunadhoofisha uwezo wetu wa kukabiliana na changamoto zinazoikumba bahari.”

Kulingana na Umoja wa Mataifa, hatari zinazoendelea kukumba mazingira ya baharini ulimwenguni zimegeuka na kuwa majanga.

Majanga haya ni pamoja na kuongezeka kwa halijoto baharini, kuongezeka kwa viwango vya asidi katika maji ya baharini, uchafuzi wa mazingira unaotokana na plastiki na uvuvi kupindukia, shughuli ambazo mbali na kuharibu mazingira ya baharini na kuathiri jamii zinazotegemea bahari, zimeendelea kuathiri uchumi katika mataifa ya mapato ya chini na ya wastani, Kenya miongoni mwao.

Maelfu ya wajumbe ikiwa ni pamoja na wanasayansi na wanaharakati wa kimazingira, waliwasili jijini Nice huku nia yao ikiwa ni kushinikiza hatua thabiti za kuhifadhi mazingira ya baharini.

Makala haya yametayarishwa kupitia usaidizi wa Association Aftica21