Korti yakataa ombi la DPP kutamatisha kesi ya ufisadi
MAHAKAMA imekataa ombi la mkurugenzi wa mashtaka ya umma (DPP) Renson Ingonga la kutamatisha kesi ya ufisadi wa Sh706milioni inayomkabili mkurugenzi wa kampuni ya uchukuzi iliyowekwa chini ya mrasimu (msimamizi aliyeteuliwa na benki) baada ya kushindwa kulipa mkopo.
Hakimu mwandamizi Bi Carolyne Nyaguthii Mugo alitupilia mbali ombi la DPP na kuamuru kesi dhidi ya Jayesh Kumar Prabudas Kotecha na kampuni yake- Midland Hauliers Limited (MHL)- (inayosimamiwa na mrasimu) akisema halina mashiko kisheria.
Bi Mugo aliagiza kesi hiyo iendelee kusikizwa Julai 15,2025 baada ya mlalamishi katika kesi hiyo Ponanigpali Venkata Ramana Rao kupinga ombi hilo la DPP vikali kupitia wakili wao Elijah Mwangi.
Akiomba kesi hiyo itamatishwe kiongozi wa mashtaka Doreen Njoroge alimweleza hakimu kwamba “ameagizwa na DPP atamatishe kesi hiyo chini ya kifungu cha sheria nambari 87(a) cha za sheria jina (CPC).
Chini ya sheria hii ya 87(a) mshukiwa akiachiliwa anaweza kamatwa tena na kushtakiwa ushahidi kamili ukipatikana.
Bw Mwangi anayemwakilisha Bw Rao aliyeteuliwa na Benki ya Prime (PBL) iliyotwaa usimamizi MHL aliambia hakimu “DPP anatumia mamlaka yake vibaya.”
Bw Mwangi alimsihi hakimu atupilie mbali ombi hilo la DPP akisema tangu 2019 yapata miaka mitano na mrasimu wa benki PBL Bw Rao amekuwa akisubiri kulipa mkopo huo wa Sh706m.
Bw Mwangi aliomba kesi hiyo itengewe siku ya kusikizwa.
Akitoa uamuzi Bi Mugo alisema kesi hiyo itaendelea kusikizwa na kuamuru kesi itajwe Julai 15,2025 kwa maagizo zaidi.
Bw Kotecha na MHL wanakabiliwa na shtaka la kula njama kuitapeli benki ya PBL Sh706,989,273 kwa kuuzia kampuni ya Super Hakika Limited (SHL) malori matatu yaliyotumika kuthamini mkopo wa Sh706milioni iliyopewa na PBL.
Bw Kotecha anakabiliwa na mashtaka matano ya kuuza dhamana bila kumwarifu mrasimu Bw Rao.
Pia ameshtakiwa kuficha habari muhimu kuhusu kampuni hiyo ya MHL.
Amekanusha mashtaka na yuko nje kwa dhamana.