Kubadilishwa kwa baadhi ya sheria katili kwawaokoa Wakenya wengi
KATIKA kipindi cha miaka miwili iliyopita, Mahakama Kuu imefuta sheria kadhaa zilizokuwa zikichukuliwa kama za kizamani, nyingi zilizotumika enzi za ukoloni na utawala wa kiimla baada ya uhuru, ambazo mara nyingi zilitumika kukandamiza uhuru wa wananchi.
Kuanzia makosa kama “kusababisha vurugu” hadi jaribio la kujiua, pamoja na vifungu katika Sheria ya Serikali na Sheria ya Urithi, mahakama zimebaini kuwa baadhi ya sheria hizo haziendani na viwango vya Katiba ya mwaka 2010.
Maamuzi haya yanachukuliwa kama ushindi mkubwa kwa Wakenya, kwani yanavunja zana za kisheria zilizokuwa zikichochea matumizi mabaya ya mamlaka ya serikali.
Mnamo Februari mwaka huu, Mahakama Kuu ilifuta kifungu cha Kanuni ya Adhabu kilichounda kosa la “kusababisha vurugu kwa namna inayoweza kutatiza amani.”
Mahakama ilisema kifungu hicho kilikuwa na tafsiri pana na isiyoeleweka, hali iliyofanya iwe vigumu kwa wananchi kujua ni vitendo gani vilivyokubalika.
Kesi hiyo iliwasilishwa na Chama cha Wanasheria nchini (LSK), kilichotaja kifungu hicho kama “masalia ya ukoloni” yaliyokiuka uhuru wa kujieleza.
Kesi hiyo ilifuatia kukamatwa kwa mwanaharakati Morara Kebaso, aliyeshtakiwa chini ya sheria hiyo baada ya kufuatilia miradi ya serikali.
Jaji Lawrence Mugambi alieleza kuwa sheria hiyo ilikuwa “zana butu” iliyolenga hata kauli halali za wananchi pamoja na vitendo halisi vya uhalifu.
Alisisitiza kuwa tayari kuna sheria mahsusi za kushughulikia vitisho vya kweli kwa usalama wa umma bila kukandamiza uhuru wa maoni.
Katika uamuzi mwingine muhimu Septemba mwaka jana, Mahakama Kuu ilifuta kifungu cha 226 cha Kanuni ya Adhabu kilichohalalisha adhabu kwa mtu anayejaribu kujiua.
Mahakama ilisema sheria hiyo ilibagua watu wenye matatizo ya afya ya akili na inakiuka haki ya utu.
Mashirika kama Tume ya Kitaifa ya Haki za Kibinadamu (KNCHR) yalieleza kuwa sheria hiyo ilikuwa ikichochea unyanyapaa na kuwazuia watu wanaohitaji msaada kutafuta matibabu.
Takwimu zinaonyesha kuwa takriban watu milioni 1.9 nchini wanakabiliwa na msongo wa mawazo, hali inayohitaji msaada badala ya adhabu.
Mahakama pia ililinda haki za wakulima kwa kufuta vifungu vya Sheria ya Mbegu vilivyokataza kuhifadhi, kubadilishana au kuuza mbegu za kienyeji.
Ilibainika kuwa sheria hiyo iliwapendelea wawekezaji wakubwa huku ikiathiri wakulima wadogo, hivyo kukiuka haki ya chakula na riziki.
Aidha, katika ushindi kwa wanaume, Mahakama Kuu ilifuta kifungu cha Sheria ya Urithi kilichomtaka mjane wa kiume kuthibitisha alikuwa akitegemea marehemu mkewe ili kurithi mali ya mwendazake, huku mjane wa kike akiruhusiwa moja kwa moja. Mahakama ilisema hilo lilikuwa ubaguzi wa kijinsia.
Katika hatua nyingine, mahakama ilifuta pia vipengele vya Sheria ya Mashauri dhidi ya Serikali vilivyoweka vizuizi kwa wananchi kufungua kesi dhidi ya serikali, ikivitaja kama sheria za kikoloni.
Maamuzi haya yanaashiria mageuzi makubwa katika mfumo wa sheria nchini, yakisisitiza umuhimu wa kulinda haki za kimsingi, usawa na uhuru wa wananchi kama ilivyobainishwa katika Katiba ya 2010.