Kukutana kisiri na katibu Raymond Omollo kulivyowaramba madiwani
JIONI ya Februari 6, 2026, baadhi ya madiwani wa kaunti ya Homa Bay walisafiri kimyakimya hadi kijiji cha Kanyipir, Karachuonyo, kwa mkutano na Katibu Mkuu wa Wizara ya Usalama wa Ndani, Raymond Omollo.
Mkutano huo uliwaleta pamoja baadhi ya wawakilishi wa wadi kutoka Homa Bay, Kisumu na Nairobi. Ingawa ulikuwa wa kijamii kwa sura ya nje, mazungumzo yake yalikuwa na uzito mkubwa wa kisiasa.
Kwa mujibu wa baadhi ya waliohudhuria, ajenda kuu ilikuwa jinsi kundi hilo lingeisaidia chama cha United Democratic Alliance (UDA) katika kampeni za kumchagua tena Rais William Ruto katika uchaguzi wa 2027. Madiwani kadhaa walisema Dkt Omollo aliwahimiza kumpigia debe Rais anayetafuta muhula wa pili.
Picha zao wakiwa katika makazi ya mashambani ya Dkt Omollo zilisambaa mitandaoni. Kwao, ulikuwa mkutano wa kawaida wa kisiasa. Hata hivyo, ndani ya Bunge la Kaunti ya Homa Bay, ziara hiyo ilitafsiriwa tofauti, kama ishara ya kutokuwa waaminifu kisiasa.
Baadaye, baadhi yao waliondolewa katika kamati mbalimbali zenye ushawishi. Uongozi wa Bunge ulieleza mabadiliko hayo kuwa ya kiutaratibu kwa lengo la kuimarisha ufanisi.
Walioathiriwa ni pamoja na Vickins Bondo (West Kasipul), Tony Otieno (Arujo), Boaz Kiri (North Kabuoch) na diwani wa kuteuliwa Pauline Omogi. Wameapa kwenda kortini kutafuta tafsiri ya mahakama kuhusu iwapo wanaweza kuondolewa kwenye kamati bila kufuata utaratibu unaofaa.
Bw Bondo alisema kuondolewa kwake kulikiuka kanuni za Bunge na hakukutokana na sababu zilizotolewa wala hakupewa nafasi ya kujitetea. Alikuwa makamu mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo ya Wadi na mwanachama wa kamati nyingine tatu.
Uanachama wa kamati si wa heshima tu; huwezesha madiwani kushughulikia masuala ya wananchi na pia huambatana na marupurupu ya kifedha.
Madiwani hao wanadai kuondolewa kwao kulijadiliwa katika kikao cha faragha na kwamba waliotajwa walionekana kama “waasi.” Wanasema kuwa kushirikiana na viongozi wa kitaifa si kosa kisheria.
Spika wa Bunge la Kaunti ya Homa Bay, Polycarp Okombo, alikanusha madai kuwa hatua hiyo ilikuwa ya kisiasa. Alisema marekebisho ya kamati yalifuata taratibu.