Lagat alemewa na presha na kuamua kukanyaga kubwa kubwa
BAADA ya kusukumiwa presha kali na Wakenya wa matabaka mbalimbali, hatimaye Naibu Inspekta Jenerali Eliud Lagat jana alijiondoa kwa muda afisini ili kutoa nafasi kwa uchunguzi unaoendelea kuhusu kifo cha bloga Albert Ojwang.
Kwenye taarifa aliyoitoa jana, Bw Lagat alisema amechukua hatua hiyo kwa kutambua wajibu wake kama Naibu Inspekta Jenerali katika Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) na “kwa sababu ya uchunguzi unaoendelea kuhusu kifo cha kusikitisha cha Albert Ojwang”.
“Leo nimeamua kujiondoa katika afisi ya Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi hadi uchunguzi unaoendelea utakapokamilika.
ajukumu ya afisi yangu kuanzia sasa yatatekelezwa na naibu wangu hadi uchunguzi utakapokamilika,” akasema.
Bw Lagat aliahidi kutoa usaidizi wowote ambao wachunguzi watahitaji watakapokuwa wakiendesha kazi yao.
“Ninatoa risala za pole kwa familia ya Albert Ojwang’ kwa kupoteza mpendwa wao,” akasema.
Uchunguzi kuhusu kisa hicho unaendeshwa na Mamlaka Huru ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (IPOA) na kufikia sasa maafisa wawili wa polisi wamekamatwa.
Wao ni Afisa Mkuu wa Kituo cha Polisi cha Central (OCS) Samson Talaam na Konstabo James Mukhwana.
Aidha, raia mmoja anayetuhumiwa kuvuruga kamera za usalama (CCTV) katika kituo cha Cental, ili kuficha ukweli kuhusu kilichomtendekea Ojwang’ akiwe seli, pia amenaswa.
Isitoshe, IPOA ilisema imewakamata wafungwa watatu, Gin Ammitoa Abwao, Collins Karani Ireri na Brian Mwaniki Njue, waliodaiwa kutumiwa na polisi kumdhulumu Ojwang’ ndani ya seli.
Kwa ujumla, IPOA imeripoti kuwa maafisa wake wamewahoji jumla ya watu 23, baadhi yao wakiwa maafisa wa polisi, kuhusiana na kifo cha bloga huyo, ambaye pia alikuwa mwalimu wa shule ya upili katika Kaunti ya Taita Taveta.
Bw Ojwang’ alikufa Juni 8, 2025 baada ya kudaiwa kudhulumiwa katika kituo cha polisi cha Central, Nairobi.
Mwendazake alikamatwa nyumbani kwao Homa Bay, baada ya Bw Lagat kuwasilisha malalamishi kwa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) kwamba aliweka mitandaoni taarifa za kumharibia jina.
Kifo cha Ojwang’ kimekasirisha umma hasa baada ya ripoti ya mwanapatholojia wa serikali kufichua kuwa alikufa baada ya kuteswa, kuchapwa kikatili na kunyongwa katika kituo cha polisi cha Central.
Awali, ripoti ya polisi ilisema alijiua kwa kugonga kichwa chake katika ukuta wa ndani ya seli ya kituo hicho alikozuiliwa baada ya kusafirishwa kutoka nyumbani kwao kijiji cha Kakoth, eneobunge la Kabondo Kasipul.
Mnamo Jumatano wiki jana, maseneta wakiongozwa na Seneta wa Homa Bay Moses Kajwang’ walimlazimisha Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja kuondoa madai hayo na akasalimu amri.
“Spika ninaondoa madai yetu ya awali kwamba Ojwang’ alikufa kutokana na majeraha aliyopata baada ya kugonga kichwa chake kwenye ukuta wa seli katika kituo cha Central. Ninaomba msamaha mwa familia ya mwendazake na Wakenya wote kwa hitilafu hiyo,” Bw Kanja akasema.
Tangu wakati huo, watetezi wa haki za binadamu, wanasiasa na raia wa kawaida wamekuwa wakishinikiza Bw Lagat ajiuzulu kuhusiana na kifo hicho cha Ojwang’.
Jaji Mkuu Mstaafu David Maraga ndiye kiongozi wa hivi punde kumtaka afisa huyo ajiuzulu kwa “kuhusishwa moja kwa moja na kifo cha Ojwang’”.
Akiongea na wahabari nje ya makao makuu ya NPS jana, Bw Maraga vilevile aliwataka Bw Kanja na Mkurugenzi wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI), Mohammed Amin kuwajibikia kifo cha bloga huyo.
“Sasa imebainika wazi kwamba Bw Eliud Lagat—kama mtu binafsi au kupitia washirika wake—ni mhusika mkuu katika kukamatwa, kuteswa, kunyongwa na hatimaye kuuawa kwa Albert Ojwang. Lakini inaudhi kuwa Bw Douglas Kanja na Bw Mohamed Amin walidanganya kuhusu suala hili hata baada ya kulishwa kiapo,” akasema.
Bw Maraga, ambaye aliongoza jopo lililotoa mapendekezo kuhusu namna ya kuimarishwa kwa maslahi ya polisi na mageuzi ya kuboresha utendakazi wa maafisa hao, alitishia kuwashtaki Kanja, Lagat na Amin, endapo hatua za kisheria hazitachukuliwa dhidi yao.
“Ikiwa hamna mashtaka yoyote yatafunguliwa dhidi ya Kanja, Lagat na Amin kufikia Juni 25, 2025, nitaanza mshtaka ya kibinafsi dhidi ya watatu hao, kwani hatua kama hiyo inakubalika kisheria,” Bw Maraga akasema huku akiikashifu serikali ya Rais William Ruto kwa kuendeleza mauaji ya kiholela.
Akitoa kauli yake kuhusu kisa hicho wiki jana, Dkt Ruto alilaani mauaji ya Ojwang’ na kuahidi kuwa hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wahusika wote wawe raia au maafisa wa polisi.
“Kwa hivyo, ninaomba IPOA kuendesha uchunguzi wa kina na kwa weledi ili ukweli kuhusu mauaji ya kijana huyo ujulikane na wahusika waadhibiwe kwa mujibu wa sheria,” akasema.
Wakati huo huo, OCS wa kituo cha Central, Bw Talaam aliyekamatwa kuhusiana na mauaji ya kinyama ya Ojwang’ alifikishwa kortini jana.
Hakimu mwandamizi wa mahakama ya Milimani, Bw Benmark Ekhubi aliamuru Bw Talaam azuiliwe katika kituo cha polisi cha Lang’ata hadi Juni 18,2025, ambapo uamuzi wa iwapo atazuiliwa kwa siku 21 au ataachiliwa kwa dhamana utatolewa.
Mawakili wanaomwakilisha afisa huyo walimsihi Bw Ekhubi aamuru uchunguzi wa kubaini kilichosababisha kifo cha Ojwang’ uongozwe na idara ya mahakama badala ya kufanywa na IPOA.
Mawakili Felix Keyton, Danstan Omari, Stanley Kang’ahi, Shadrack Wambui, Cliff Ombeta miongoni mwa wengine walisema,
“Itakuwa vigumu maafisa wa polisi kufichua vitendo vya wenzao chini ya mwongozo wa kutofanya ufichuzi almaarufu Blue Code of Silence (BCS).”
Bw Keyton aliomba hakimu amwachilie Bw Talaam kwa dhamana ya Sh7,000 pesa tasilimu na kumwamuru asiende katika kituo cha polisi cha Central.
“Bw Talaam alisimamishwa kazi na kuamriwa awe akipiga ripoti kwa afisa msimamizi wa kituo cha polisi cha Eldoret,” Bw Keyton alimweleza hakimu.
Bw Keyton alieleza hakimu kwamba Bw Talaam alijisalimisha kwa maafisa wa uchunguzi wa jinai (DCI) mnamo Juni 13,2025 na kwamba atatii na kufuata masharti atakayoagizwa na mahakama.
Bw Omari alieleza mahakama kwamba Bw Talaam ametumikia kikosi cha polisi kwa muda wa miaka 29 hivyo basi “hana rekodi yoyote ya uhalifu.”
Bw Omari aliomba mahakama iamuru mauaji hayo ya kinyama ya Ojwang’ yachunguzwe na mahakama kwa vile “hakutakuwa na visa vya kuuficha ukweli”.
Bw Omari alieleza mahakama kwamba DIG Eliud Lagat ndiye ametajwa na kila mtu kwamba alilalamika kwa DCI baada ya Ojwang’ kuchapisha habari mbaya kumhusu katika mitandao ya kijamii.