LSK yamkemea Murkomen kwa matamshi yake
CHAMA cha Mawakili Nchini (LSK) kimemshutumu Waziri wa Usalama Kipchumba Murkomen kwa kuwaagiza polisi wawapige risasi raia watakaovamia vituo vya polisi nchini.
Kwenye taarifa Ijumaa, Juni 27, 2025 Rais wa LSK Faith Odhiambo alisema Bw Murkomen hana mamlaka kisheria na kikatiba kitoa amri kama hiyo bali Inspekta Mkuu wa Polisi Douglas Kanja.
“Amri hiyo ni haramu na inakwenda kinyume cha Katiba. Kwa hivyo, LSK inaonya maafisa wa polisi dhidi ya kutii agizo kama hilo kwani wasije wakaandamwa na mkono wa sheria,” akasema.
“Kulingana na Sheria ya Huduma ya Kitaifa ya Polisi (NPS) ni Inspekta Jenerali wa Polisi pekee aliye na mamlaka ya kutoa agizo kama hilo la kioperesheni. Na Inspekta Jenerali hafai kupata ushauri kutoka kwa yoyote anapotoa agizo kama hilo au lingine kwa maafisa wa polisi wanaohudumu chini yake,” Bi Odhiambo akaongeza.
Rais huyo wa LSK alimkumbusho Waziri Murkomen kwamba ni juzi tu ambapo aliwaambia wabunge na maseneta kwamba afisi yake haina wajibu wa kutoa maagizo kwa polisi kuhusu kile wanapasa kufanya au la.
“Juzi, Murkomen aliambia Bunge la Kitaifa na lile la Seneti kwamba afisi yake haina mamlaka ya kutoa maagizo kwa Inspekta Jenerali wa Polisi na Huduma ya Kitaifa ya Polisi. Sasa iweje kwamba anawaagiza polisi kuwapiga raia risasi wakithubuti kufika katika vituo vya polisi?”, Bi Odhiambo akauliza.
Rais huyo wa LSK alisema haki ya mtu kuishi inalindwa na Katiba na hakuna mtu aliye na mamlaka ya kuondoa maisha ya mtu mwingine ila chini ya sheria maalum.
Bi Odhiambo alionya kwamba matumizi ya nguvu kupita kiasi na mauaji yoyote ya kiholela kwa kizingizio cha kufuata agizo la Murkomen, yatachukuliwa kama uhalifu wa kukusudia.
Rais huyo wa LSK alimtaka Inspekta Jenerali wa Polisi Kanja kuingilia kati na kuhakikisha kuwa maafisa wake hawachelei kuzingatia wajibu wao wa kikatiba kwa kutii amri haramu.
“Afisa yoyote atakayethubutu kutenda uhalifu kama huo atashtakiwa kama mtu binafsi. Vile vile, Inspekta Jenerali wa polisi ataelekezewa lawama kwa hilo,” Bi Odhiambo akaeleza.
Mnamo Alhalisi, Juni 26, 2025 Bw Murkomen alitoa amri kwa polisi kuwaua kwa kuwapiga risasi wananchi watakaodhubutu kuvamia vituo vya polisi.
“Mtu yeyote atakayekaribia kituo cha polisi apigwe risasi. Bunduki ambazo polisi hupewa sio fimbo bali ni silaha ya kutumia panapohitajika, Bw Murkomen akasema katika kituo cha polisi cha Kikuyu kilichoteketezwa na wahuni wakati wa maandamano ya Jumatano.
Hata hivyo, wananchi waliokuwa wakimsikiziwa walimzomea kwa kutoa kauli kama hiyo baadhi yao wakimpendekeza kuwa wahalifu wakamatwe na kushtakiwa kwa mujibu wa sheria badala ya kuuawa.
Baadaye Ijumaa, Bw Murkomen alifafanua kwamba amri yake ililenga wahalifu wanaojaribu kutekeleza wizi katika vituo vya polisi na kuwajeruhi maafisa bali sio agizo lililohusu aina zote za tishio.
Waziri alisema kuwa lengo lake lilikuwa ni kulinda maafisa wa polisi na mali ya umma katika vituo vya polisi isiharibiwe au kuibiwa na wahalifu.
Hata hivyo, mashirika ya kutetea haki za kibinadamu, wanasheria, wanasiasa wa upinzani na Wakenya kwa ujumla walishikilia kuwa agizo la Bw Murkomen linaweza kuongeza visa vya polisi kutumia nguvu kupitia kiasi na kuwaua raia kiholela.