Habari

Maafisa watatu wakuu kujiuzulu kutokana na kashfa ya mafuta yenye thamani ya Sh4.8b

Na STEVE OTIENO na KAMORE MAINA April 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAAFISA wanne wakuu kutoka Wizara ya Kawi, Mamlaka ya Udhibiti wa Kawi na Petroli (EPRA) na Kampuni ya Mabomba ya Kenya (KPC) kujiuzulu kutokana na kashfa ya mafuta yenye thamani ya Sh4.8 bilioni.

Katibu wa Kawi, Mohammed Liban; Mkurugenzi Mkuu wa EPRA, Daniel Kiptoo; Mkurugenzi Mtendaji wa KPC, Joe Sang; pamoja na mfanyakazi wake, Simon Wafula, walikamatwa na maafisa wa Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI).

Walizuiliwa katika vituo mbalimbali vya polisi kabla ya kupelekwa makao makuu ya DCI kwenye barabara ya Kiambu jana mchana.

DCI pia inatafuta maafisa wengine kama sehemu ya uchunguzi mpana kuhusu kile kinachoshukiwa kuwa kuvuruga mfumo wa usambazaji wa mafuta.

Vyanzo vinasema operesheni hiyo ilianza Alhamisi usiku, na mali na stakabadhi zilichukuliwa nyumbani kwa washukiwa ili kusaidia katika uchunguzi.

Uchunguzi unazingatia madai kwamba shehena ya mafuta chini ya makubaliano ya serikali-kwa-serikali (G-to-G) ilizuiwa kwa dai linalohusiana na ubora wake , hali iliyosababisha hofu ya uhaba wa bidhaa.

Ilidaiwa kuwa shehena hiyo ilikuwa na viwango vya juu vya madini hatari ambavyo havikubaliki Kenya, jambo lililosababisha maswali kuhusu matumizi yake sokoni.

Meneja wa uhakiki wa ubora wa KPC aliyekagua mafuta hayo alizuia usambazaji na kuarifu mamlaka kuhusu tatizo hilo, hatua iliyosababisha shinikizo la ndani na mzozo kuhusu iwapo bidhaa hiyo ingetolewa sokoni, kabla ya suala kufikishwa kwa wakaguzi.

Hali hii inajitokeza huku taifa likikabiliwa na hofu kuhusu uthabiti wa usambazaji wa mafuta. Kenya inategemea sana wasambazaji wa mafuta kutoka Ghuba ikiwemo Saudi Aramco, Abu Dhabi National Oil Company (ADNOC) na Emirates National Oil Company (ENOC) kupitia makubaliano ya serikali-kwa-serikali.

Makubaliano haya yameongezwa muda hadi mwaka wa fedha 2027/2028 na yamekuwa muhimu kukinga taifa dhidi ya mabadiliko ya bei za mafuta duniani.Kabla ya hatua hii , Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi, aliambia Seneti kwamba kampuni za kimataifa zinazotoa mafuta nchini zimeruhusiwa kununua bidhaa nje ya Mashariki ya Kati.

Alitoa agizo kwa wauzaji wa mafuta kuachilia mafuta yaliyohifadhiwa sokoni, akionya kuwa kushikilia bidhaa ni kinyume cha sheria na maslahi ya umma.

Wakati huohuo, Waziri wa Fedha na Mpango wa Kitaifa, John Mbadi, alihakikisha wananchi kuna usambazaji thabiti wa mafuta., akisema hifadhi za sasa zinatosha kwa siku 16 za petroli, 19 za dizeli, na 49 za mafuta ya ndege na taa.

Aliongeza kuwa mzunguko wa bei wa sasa haupaswi kuathirika mara moja kutokana na mzozo wa Mashariki ya Kati, kwani shehena zilizopokelewa kabla ya mzozo ni salama.