Maandamano yazuka tena Nairobi
POLISI Jumanne Juni 17, 2025 walilazimika kutumia vitoa machozi kuwatawanya waandamanaji waliojitokeza katikati mwa jiji la Nairobi kudai haki na fidia kwa vijana wa GenZ waliouawa kikatili na polisi.
Hii ni baada ya waandamanaji hao kujikusanya nje ya jengo la Nation Center kufanya maombi kabla ya kuanza maandamano yao rasmi.
Pindi tu walipomaliza kuomba, maafisa wa polisi waliwarushia vitoa machozi kuwatawanya.
Hali hii ilifanya baadhi ya wafanyabiashara kufunga maduka yao kwa hofu ya kuporwa kama ilivyotokea wiki jana wakati wa maandamano ya kutaka haki kwa mwalimu-bloga Albert Ojwang aliyeaga dunia mikononi mwa polisi.
Kumekuwa na visa vya watu kutekwa nyara na kuuawa kiholela mikononi mwa polisi.
Kulingana na ripoti iliyotolewa Septemba mwaka jana na Amnesty International na mashirika kadhaa ya haki za binadamu vijana wengi waliangamia na wengine kutekwa nyara wakati wa maandamano ya vijana wa Gen Z ya ‘Occupy Parliament’ yaliyofanyika Juni 25, 2024.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo iliyotokana na utafiti na mahojiano ya kina, watu 61 waliuawa na wengine 72 walitekwa nyara au hawajulikani waliko kutokana na maandamano hayo.
Baadhi ya familia ya waathiriwa hazijapata haki hadi sasa na hii ndio maana watu wamejitokeza jijini Nairobi kuandamana.