Maasi ya Gen Z yatia hofu vigogo wa siasa za kimaeneo nchini
VIGOGO wa kieneo wa kisiasa nchini ambao kwa kawaida wamekuwa wakijivunia ufuasi mkubwa, sasa wapo hatarini kupoteza umaarufu huo kutokana na kuchipuka kwa maasi ya Gen Z dhidi ya serikali.
Mnamo Jumatano wiki jana, halaiki ya vijana walimwaagika barabarani katika zaidi ya kaunti 27 kwa maadhimisho ya mwaka moja tangu tukio la kihistoria la kuvamiwa kwa bunge mnamo Juni 25, 2024.
Wakiwa walizaliwa kati ya mapema miaka ya 90s na 2010, vijana hao wanaelekea kulemaza vigogo wa kisasa ambao wamekuwa na ushawishi katika siasa za nchi kwa miaka mingi.
Kufanikisha maasi dhidi ya serikali, wamekuwa wakitumia mitandao ya kijamii na majukwaa mbalimbali ya kidijitali kupigania haki yao.
Rais William Ruto, Kinara wa ODM Raila Odinga, Kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka na Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta ni kati ya wanasiasa ambao wamekuwa wafalme wa kisiasa katika jamii na maeneo yao.
Hata katika chaguzi za nyuma, vigogo hao wamekuwa na ushawishi kwenye jamii zao huku wakizoa kura nyingi.
Kwenye uchaguzi wa 2013, Rais Ruto na Bw Kenyatta walitegemea sana mawimbi ya kisiasa ya jamii zao eneo la Bonde la Ufa na Mlima Kenya kuwahi uongozi wa nchi.
Hata hivyo, maandamano ya Gen Z na umoja ambao wameudhirisha dhidi ya uongozi usioridhisha nchini, sasa unaashiria kuwa mibabe wa kisiasa nchini wanaelekea kupoteza udhabiti wao.
“Gen Z huenda wakalemaza vigogo hao wa kieneo na hawatakuwa na ushawishi kama hapo awali. Hawawatambui na jinsi wanavyoendelea, huenda wakawa na ushawishi mkubwa kwenye uchaguzi mkuu wa 2027,” akasema Profesa Macharia Munene, ambaye ni mhadhiri na mchanganuzi wa masuala ya kisiasa.
Kwa miaka mingi, Bw Odinga amekuwa sura ya maandamano nchini huku akitikisa tawala zilizopita. Hata hivyo, maandamano ya Juni 25, 2024 na Juni 25, 2025 yameonyesha kuwa bila hata Raila, Gen Z wanaweza kutetemesha serikali.
Mwaka jana, waandamanaji walimwaambia Bw Odinga akae nyumbani lakini baada ya kujiunga na serikali, walimkejeli kwa kulemaza juhudi zao na kula na watesi wao.
Wiki jana, baadhi walimkejeli Raila wakisema maandamano yao yamefaulu hata bila uungwaji mkono wake.
Kufikia mnamo 2027, wengi wa Gen Z watakuwa wamefikisha umri wa kupiga kura. Shirika la Takwimu Nchini (KNBS) linaonyesha kuwa zaidi ya Gen Z milioni 14 watakuwa wamefikisha umri wa kupiga kura.
Kwenye kura ya 2022, idadi yao ndogo ndiyo ilitokea kwa mujibu wa Takwimu za Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC).
Sajili ya kura ya 2022 inaonyesha kuwa kulikuwa na wapigakura 8,811,691 ambao walikuwa kati umri wa miaka 18-34 ambayo ilikuwa asilimia 40 ya kura zote.
Kufikia 2027 Wakenya ambao wapo kati ya umri wa miaka 18 hadi miaka 34 watakuwa zaidi ya milioni 17.8 na hii itawapa nafasi nzuri ya kuamua mustakabali ya nchi.
Seneta wa Kitui Enoch Wambua alisema kuwa Gen Z wakitumia vyema takwimu zao, watabadilisha uongozi wa nchi hii.
“Hili ni kundi ambalo linaongozwa na kiu cha uongozi bora baada ya kupitia kipindi kigumu. Sasa wanataka uwajibikaji bila kutumia ukabila ambao umekuwa nguzo ya baadhi ya wanasiasa kuendeleza maslahi na ajenda zao,” akasema Bw Wambua.
Mtaalamu wa Masuala ya Uongozi Javas Bigambo alisema maandamano yameonyesha kuwa vijana wana kiu na ari ya kuchukua uongozi wa nchi.
“Wale ambao wapo mamlakani hawafai kuwapuuza. Ubunifu wao na juhudi wanazofanya kushinikiza mabadiliko yanastahili kuwatia wasiwasi viongozi debeni,” akasema Bw Bigambo.