Habari

Mabunge 13 yamulikwa kuhusiana na mamilioni ya nyumba za maspika

Na VITALIS KIMUTAI June 25th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MKAGUZI Mkuu wa Hesabu za Serikali ameorodhesha mabunge 13 ya kaunti ambayo hayajakamilisha ujenzi wa makazi rasmi ya Spika wa Bunge la Kaunti miaka mitatu baada ya muda uliowekwa na Serikali Kuu mwaka 2022 kupita.

Ujenzi wa nyumba hizo ulikuwa wa kima cha Sh36 milioni kwa kila nyumba kama ilivyowekwa na Tume ya Mishahara na Marupurupu (SRC), lakini ukaguzi umeonyesha gharama inaweza kuzidi kiasi cha Sh455 milioni.

Mnamo Oktoba 24 2016, SRC iliandikia mabunge yote ya kaunti ikiyashauri yapatie kipaumbele ujenzi wa makazi ya Spika katika bajeti ya 2018/2019 na ikaweka Juni30, 2022 kuwa tarehe ya mwisho ya miradi hiyo kukamilika.

Hata hivyo, ripoti za ukaguzi zinaonyesha baadhi ya mabunge hayajatekeleza agizo hilo.Baadhi ya mabunge ya kaunti yamepitisha fedha za bajeti zilizopangwa, huku baadhi ya maspika wakipata marupurupu ya kukodisha nyumba ingawa wanaishi katika makazi rasmi.

Muda wa kukamilisha ujenzi huo umeongezwa angalau mara sita katika baadhi ya kaunti na wanakandarasi wengi wamekataa kuendelea na kazi.

“Baadhi ya mabunge yamejenga nyumba hizo katika ardhi ya kibinafsi, kinyume cha sheria,” alisema Mkaguzi Mkuu, Bi Nancy Gathungu.

Kaunti ambazo hazijatekeleza maagizo ya SRC ni: Vihiga, Kericho, Nyandarua, Tana River, Marsabit, Uasin Gishu, Mandera, Tharaka Nithi, Homa Bay, Kisumu, Kisii, Nyamira na Busia.

“Kukosa kukamilisha miradi kunaweza kusababisha ongezeko la gharama kutokana na mabadiliko ya bei ya vifaa na huduma,” alisema Bi Gathungu katika ripoti yake ya 2023/2024.

Kulingana na ripoti ya ukaguzi, Bunge la Kaunti ya Kericho tayari limezidisha bajeti kwa kiasi cha Sh11.3 milioni huku Bunge la Kaunti ya Vihiga likizidisha kwa Sh4.1 milioni.

Katika Kaunti ya Marsabit, Spika alilipwa Sh900,000 kwa kukodisha nyumba, ingawa hakutoa mkataba wa kukodisha kwa ukaguzi.

“Hakukuwa na maelezo kwanini ujenzi haujakamilika na kwa nini Bunge la Kaunti liliendelea kulipa kodi ya kukodisha nyumba licha ya mkataba kuisha Juni 30, 2022,” alisema Bi Gathungu.

Spika wa Bunge la Vihiga alipokea kitita ambacho hakikufafanuliwa licha ya kuishi katika nyumba rasmi iliyokamilika kwa gharama ya Sh38,681,697.

“Gharama ya Makazi ya Spika ilipita kiasi cha Sh34,493,609 kwa Sh4,186,944 bila kibali cha kufanyia kandarasi marekebisho,” alisema Bi Gathungu.

Makazi hayo yaliwekwa ukuta, bustani, choo cha nje, kisima, mapambo ya ndani, na fanicha –zote kwa gharama inayozidi iliyowekwa kisheria.

Kufikia Juni 30, 2024, Bunge la Vihiga lilitumia Sh73,446,130 dhidi ya kiwango cha Sh35 milioni kilichowekwa Mei 2019.

Nyumba hiyo imejengwa katika eneo la ekari 2.87  ilhali sheria inasema ekari moja tu, na eneo lilinunuliwa kutoka kwa mtu binafsi licha ya kuwa mali ya serikali ya kaunti.

Pia hakuna hatimiliki iliyotolewa wakati wa ukaguzi, hitaji muhimu kwa vibali vya NEMA.

Katika kaunti ya Kericho, tarehe ya kukamilika kwa ujenzi wa nyumba ya spika imerekebishwa mara sita ndani ya miaka saba, na gharama kuongezeka kwa Sh11,369,710.

Bunge la Nyandarua pia lilipitisha muda uliowekwa na SRC kwa kununua ekari 1.7 badala ya ekari moja, na kujenga ukuta kinyume cha sheria.

Bunge la Uasin Gishu lilitia mkataba wa Sh34,850,935 uliopaswa kuchukua miezi 72, lakini hadi Septemba 2024 ujenzi uko ulikuwa asilimia 40.

Kaunti ya Tharaka Nithi nyumba ya spika ilikuwa imekamilika asilimia 56.7 tu kufikia Juni 30, 2024.

Tana River, Mandera, Bomet, Kisumu, Homa Bay, Kisii, na Nyamira zote zimeonekana kushindwa kukamilisha mradi huo kwa wakati.

Baadhi ya wanakandarasi wameacha kazi ikiwa bado kukamilika.