Mackenzie pabaya mshirika wake akikiri makosa 43
MHUBIRI tata Paul Mackenzie amepata pigo jingine baada ya mkuu wa “usalama” wa Shakahola wakati wa ‘kuomba na kufunga’ uliosababisha vifo vya zaidi ya waumini 450 wa kanisa lake kukiri kosa katika kesi ya kuua bila kukusudia.
Enos Amanya Ngala, maarufu kama “Hallelujah,” jana alifikishwa tena mahakamani na kushtakiwa upya kwa makosa 43 ya kuua bila kukusudia kufuatia makubaliano na upande wa mashtaka.
Chini ya makubaliano hayo, Amanya alikiri makosa yote 43 kwa hiari yake, akithibitishia mahakama kuwa uamuzi wake haukuchochewa na vitisho, shinikizo wala ushawishi wa aina yoyote.
Kama sehemu ya makubaliano hayo, Amanya alikubali kutoa taarifa kamili na za ukweli pamoja na kushirikiana na upande wa mashtaka.
Hii inajumuisha kurekodi taarifa ya ushahidi kwa wachunguzi na kutoa ushahidi kama shahidi wa upande wa mashtaka katika kesi inayoendelea ya mauaji ya Shakahola, ikiwemo tukio la Kwa Bi Nzaro.
Aidha, Amanya, ambaye alipoteza watoto wake sita katika eneo hilo kutokana na mafundisho potovu wa Shakahola uliowahusisha zaidi ya waumini 450 wa kanisa la Good News International, alikubali kushiriki kwa hiari katika mpango maalum wa urekebishaji wakati wa kifungo chake.
Serikali, kupitia Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP), ilikubali kuondoa mashtaka 195 kati ya mashtaka 238 ya awali ya kuua bila kukusudia yaliyokuwa yakimkabili Amanya.
Kama sehemu ya makubaliano hayo, upande wa mashtaka pia uliahidi kuondoa mashtaka yote yaliyokuwa yakimkabili katika Mahakama ya Watoto ya Tononoka.
“Tunaomba mahakama imchukulie Amanya kama mkosaji wa mara ya kwanza na isimhukumu kifungo cha juu kabisa cha jela cha maisha,” upande wa mashtaka uliwasilisha.
Badala yake, upande wa mashtaka ulipendekeza kifungo cha miaka kumi na moja gerezani, kwa kuzingatia miaka mitatu ambayo tayari ameitumikia akiwa rumande.
Zaidi ya hayo, miaka minane iliyosalia itajumuisha miaka miwili ya kifungo chini ya mpango wa urekebishaji unaoendeshwa na Idara ya Magereza pamoja na Kituo cha Kitaifa cha Kupambana na Ugaidi, ikifuatiwa na miaka sita ya kifungo cha nje chini ya uangalizi wa maafisa kwa ajili ya kumrejesha katika jamii.
Amanya alithibitisha kuwa alielewa kikamilifu masharti ya makubaliano hayo kabla ya kuweka saini yake.
Makubaliano hayo yalifikiwa baada ya zaidi ya mashahidi 100 kutoa ushahidi katika kesi ya kuua bila kukusudia ambapo washukiwa walikuwa wakikabiliwa na mashtaka 238.
Licha ya hatua hiyo ya Amanya, mkewe, Anne Anyoso, na nduguye mdogo, David Amanya, wameendelea kukana mashtaka dhidi yao.
Makubaliano hayo sasa yanaimarisha kesi ya upande wa mashtaka dhidi ya washtakiwa waliosalia, kwa kuwa Amanya, akiwa mtu wa ndani, anatarajiwa kueleza mahakamani kilichotokea ndani ya msitu huo na waliokuwa wamehusika katika vifo vya zaidi ya waumini 450 wa kanisa hilo lililopigwa marufuku.
Awali, katika kesi ya mauaji iliyokuwa ikiendelea dhidi yao ambapo Amanya pia alikuwa amekiri kosa, aliieleza mahakama jinsi Mackenzie alivyoanzisha mfungo ndani ya msitu huo baada ya kubainika kwamba walikuwa wanakaribia kufukuzwa kutoka eneo hilo.
Aliiambia mahakama kuwa walikuwa zaidi ya watu 1,000 ndani ya msitu huo na kwamba takriban watu 700 au zaidi walifariki katika mfungo huo wa mauti.
Hata hivyo, takwimu zilizowasilishwa na mamlaka zinaonyesha kuwa Serikali ilifanikiwa kufukua miili ya watu 450 pekee, huku zaidi ya watu 300 wakidaiwa kuzikwa katika makaburi ya kina kifupi ndani ya msitu huo.