Madalali waendea helikopta na magari ya Didmus Barasa
HUENDA helikopta na magari sita yanayomilikiwa na Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa yakapigwa mnada kutokana na deni la Sh4.4 milioni anazodaiwa na kampuni ya mawakili.
Betico Auctioneers wanalenga helikopta hiyo na kuiwekea thamani ya Sh2 milioni, pamoja na magari sita yenye thamani ya kati ya Sh500,000 na Sh1 milioni, na pia vifaa vya nyumbani, kufuatia deni linalodaiwa na kampuni ya mawakili ya Nchogu Omwanza & Nyasimi Advocates.
Kampuni hiyo ya mawakili ilimwakilisha Bw Barasa katika kesi ya kupinga ushindi wake iliyowasilishwa katika Mahakama Kuu ya Bungoma na wakili Bryan Khaemba, mwaka wa 2022.
“Tumeorodhesha mali inayohamishika ya mdaiwa na tumeiacha chini ya uangalizi wake kwa muda wa siku saba kuanzia tarehe ya notisi hii. Baada ya hapo, tutaiondoa na kuipeleka katika yadi yetu kuuza ili kurejesha kiasi kinachodaiwa pamoja na gharama yetu,” ilisema notisi ya dalali.
Stakabadhi zilizowasilishwa mahakamani zinaonyesha kuwa Bw Barasa alimwajiri wakili huyo kumwakilisha katika kesi hiyo ya kupinga ushindi wake, na walikubaliana malipo ya Sh5 milioni.
Wakili Omwanza Ombati alisema kuwa Bw Barasa alilipa malipo ya Sh1 milioni.
Aliongeza kuwa kampuni ya mawakili ilitekeleza kazi kwa uaminifu na mafanikio, na kesi hiyo ilitupiliwa mbali kupitia uamuzi uliotolewa Novemba 22, 2022.
Bw Ombati alisema kuwa alijaribu mara kadhaa kupata kiasi kilichosalia cha Sh4 milioni bila mafanikio.
Baadaye kampuni hiyo ya mawakili iliwasilisha kesi mahakamani na kupata hukumu dhidi ya mbunge huyo.
Katika utetezi wake, Bw Barasa alisema kuwa mawakili hao hawakustahili kulipwa kiasi kilichosalia kwa kuwa kesi haikuendelea hadi kusikilizwa kikamilifu bali ilitupwa katika hatua ya awali.
Katika uamuzi uliotolewa Desemba mwaka jana, Jaji Josephine Mong’are alisema kuwa mahakama iliridhishwa na hoja zilizowasilishwa na mawakili kwamba ada zao zilistahili kulipwa mara baada ya kampuni hiyo kukubali kumwakilisha mteja na kuanza kutoa huduma.
Jaji huyo aliongeza kuwa utetezi wa Bw Barasa haukuwa na msingi na ulikuwa wa kukanusha tu bila hoja za msingi za kesi.
“Nabaini na kushikilia kuwa salio la ada ya Sh4 milioni linastahili kulipwa mawakili kulingana na makubaliano ya ada kati ya wakili na mteja,” alisema jaji.
Kampuni hiyo ya mawakili sasa inadai Sh4.46 milioni ambazo zinajumuisha riba ya Sh466,410.