Madiwani sasa hawataki mishahara yao ipitie kaunti huku njaa ikiwasakama
MADIWANI sasa wanataka mishahara itoke moja kwa moja kutoka Hazina Kuu ya Kifedha badala ya hali ya sasa ambapo inapitia kwenye kaunti.
Katika mkutano na Kamati ya Ustawi wa Kieneo kwenye Bunge la Kitaifa, madiwani walisema wanahitaji kujitegemea kifedha ili kuhepa hali ambapo mishahara yao hucheleshwa kimakusudi kutokana na tofauti zao na uongozi wa kaunti.
Mishahara ya madiwani hupitia wizara ya fedha ya kaunti na waliambia kamati hiyo inayoongozwa na Mbunge wa Sigor Peter Lochakapong kuwa wanataka Mswada kuhusu Uhusiano wa Serikali za Kaunti na Kuu 2024 upitishwe ili wawe na uhuru wa kupokea mishahara yao na wasimamie bajeti ya shughuli zao.
“Huwa hatuwezi kupata hela zetu hadi pale waziri wa kaunti aidhinishe. Hii ni licha ya kuwa hatuna bajeti ya maendeleo ila tu ya shughuli zetu. Tunasaka uhuru wa fedha,” akasema Chege Mwaura, Katibu wa Muungano wa Mabunge ya Kaunti (CAF).
Bw Mwaura alisema kuwa mabunge ya kaunti yanastahili kuwa na bajeti yao ambayo haidhibitiwi na kaunti kuhakikisha kuwa shughuli zao haziingiliwi na wakuu wa magatuzi yao.
Wanachama wa kamati hiyo wakiongozwa na Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Mandera Kassim Umul Ker Sheikh ambaye alihudumu mihula miwili kama diwani, alianika wazi changamoto za kifedha ambazo madiwani hupitia.
“Madiwani huwa hawana namna kwa sababu wanawasubiri magavana wawape ufadhili. Wanahitaji kuwa na bajeti yao ili waendelee na shughuli zao bila tatizo lolote,” akasema Bi Umul.
Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Embu Pamela Njoki Njeru pia alisema hali ambapo madiwani wanapitia kifedha kuwa mbaya.
“Madiwani wanateseka kwa sababu wakikosana na gavana ama waziri wa fedha wa kaunti, kila kitu kinasimamishwa. Tunahitaji kukomesha hilo,” akasema.
“Wanayazuia mabunge ya kaunti kufanya kazi zao ilhali wanastahili kuwawajibikia. Ni kinaya kuwa madiwani huwapiga msasa mawaziri kisha baadaye wahangaishwe na mawaziri hao,” akaongeza.
Kwa sasa wawakilishi wadi katika Kaunti ya Kirinyaga hawajapokea mshahara wo na hii inaonyesha jinsi kutegemea kaunti kunawatatiza.
Wawakilishi wadi wengi wanaandamwa na madeni, wanateseka kukithi mahitaji ya familia zao na kuwalipia watoto wao karo.
“Madiwani hawajalipwa miezi mitatu na wanahangaika sana,” akasema Naibu Spika wa Kirinyaga Jinaro Njamumo.
Bw Njamumo ambaye ni diwani wa wadi ya Mutithi akiongea mjini Kirinyaga wakati wa ibada wikendi, aliwataka Wakenya na maaskofu wawaombee ili hali yao ya kifedha iimarike.
Imebainika kuwa hata wafanyakazi wa bunge hilo la kaunti pia hawajalipwa kwa miezi mitatu.
“Wengine wetu hawajalipa kodi za nyumba na karo kwa watoto wetu,” mfanyakazi mmoja wa Bunge la Kaunti ya Kirinyaga ambaye hakutaka jina lake linukuliwe akaambia Taifa Leo.