Habari

Mahakama yaruhusu dadake Uhuru kutimua aliyekuwa mwenzi wake

Na BENSON WAMBUGU June 29th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MAHAKAMA Kuu imemruhusu Anne Nyokabi, dadake Rais mstaafu Uhuru Kenyatta, kumfurusha aliyekuwa mwenzi na mshirika wake wa kibiashara, Moses Gachemi Nderitu, kutoka kwa nyumba ambayo anadai alichangia kujenga.

Jaji Jane Onyango wa Mahakama ya Mazingira na Ardhi mjini Thika alisema kwamba ingawa Nderitu aliwasilisha kesi yenye hoja nzito na uwezekano mkubwa wa kufaulu, alishindwa kuishawishi mahakama kuwa hakuwa na uwezo wa kupata makazi mbadala.

“Nderitu hakuonyesha kuwa Bi Nyokabi alikuwa na nia ya kuuza au kutwaa nyumba hiyo kwa njia yoyote. Pia hakuweza kuthibitisha kuwa angelipata hasara isiyoweza kufidiwa kwa pesa endapo hangepewa agizo aliloomba kuzuia asitimuliwe,” alisema Jaji Onyango.

Katika kesi hiyo iliyowasilishwa Septemba 2024, Nderitu anataka mahakama iamue kwamba Nyokabi alikuwa anashikilia baadhi ya maeneo ya ardhi iliyosajiliwa kama L.R 26680/2 na L.R 26680/5 kwa niaba yake.

Alitaka pia amri ya kumzuia Nyokabi kuingilia au kumtimua kutoka nyumba au kumzuia kuendelea kuishi humo.

Kwa mujibu wa ushahidi wake, Nderitu alisema alikutana na Nyokabi mwaka wa 2002, ambapo walianzisha uhusiano wa karibu wa kibinafsi na kibiashara. Mwaka wa 2014, waliunda kampuni iitwayo KOTO Housing Kenya Limited, ambapo yeye alikuwa Mkurugenzi Mkuu.

“Baadaye tuliamua kujenga nyumba ya kifahari ambayo ilikuwa iwe makazi yetu ya pamoja,” alisema Nderitu.

Aliongeza kuwa alihusika kwa kina katika kila hatua ya ujenzi kuanzia kupanga, kupata vibali vya ujenzi, kuajiri wasanifu majengo na wahandisi, hadi ujenzi ukaanza rasmi. Alidai kuwa alitumia akiba zake zote alizopata akiwa mwanachama wa bodi ya NTSA na Mkurugenzi wa KOTO Limited kufadhili ujenzi huo.

Aidha, alichukua mkopo binafsi wa Sh6 milioni na akasema alitumia jumla ya Sh16 milioni kwa mradi huo.

Nderitu aliingia kwenye nyumba hiyo Mei 2020 ingawa haikuwa imekamilika kabisa. Hata hivyo, alijiuzulu kutoka kampuni ya KOTO Housing mnamo Juni 2020 baada ya janga la Covid-19 kuathiri kampuni hiyo kifedha. Alisema hali hiyo ilisababisha mgogoro kati yao na kupelekea uhusiano wao kuvunjika.

Mnamo Desemba 2020, Nyokabi aliandaa mkataba wa upangaji na kumwita Nderitu mpangaji, akimwarifu kuwa anaweza kuishi humo bure kwa miaka miwili kama njia ya kufidia mchango wake kwa ujenzi huo.

Hata hivyo, Nderitu alikataa kusaini mkataba huo kwa misingi kuwa hakuwa mpangaji, bali alikuwa mshirika aliyetoa mchango mkubwa wa kifedha katika mradi huo.

Jaji Onyango alibainisha kuwa Nyokabi alikiri kuwa aliwahi kuwa na uhusiano wa karibu na Nderitu, na kwa msingi huo alimruhusu kuishi kwenye nyumba hiyo kwa miaka miwili “kwa kuzingatia mchango wake katika ujenzi wa nyumba hiyo.”

Hata hivyo, Jaji alisema suala la mchango wake haliko wazi na litahitaji kusikilizwa kwa kina ili kubainisha ukweli.

Kwa sasa, Nyokabi ana uhuru wa kumtimua Nderitu kwenye nyumba hiyo, huku kesi kuhusu umiliki na mchango ikisubiri kusikilizwa kwa kina.