Habari

Mahasla ndio wanajenga nchi

Na ELVIS ONDIEK February 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WAFANYAKAZI wa tabaka la kati nchini wanakabiliwa na nyakati ngumu zijazo mishahara yao ikizidi kudorora kutokana na nyongeza ya makato, huku maskini wakiathirika pakubwa, wataalamu wa masuala ya uchumi wameonya.
Kuanzia mwezi huu wa Februari, Wakenya wanaolipwa mishahara wanatazamiwa kuathirika zaidi wakishurutishwa kuchangia zaidi kwa Hazina ya Malipo ya Uzeeeni (NSSF), makato ya asilimia 12 kwa kila mwajiriwa.
Huku wafanyakazi waking’ang’ana na mishahara inayozidi kudorora, wataalam wa uchumi wanaamini tabaka la juu linalojumuisha matajiri halijaathirika sana, maskini wakitaabika zaidi.
Sehemu kubwa ya wafanyakazi katika sekta rasmi nchini inajumuisha tabaka la kati ambalo, kando na kuwa uti wa mgongo wa viwanda mbalimbali, wanachangia sehemu kubwa ya ushuru unaokusanywa nchini.
“Ndio pekee waliosalia, wanaowasitiri maskini,” asema Profesa XN Iraki wa Chuo Kikuu cha Nairobi, Idara ya Sayansi ya Usimamizi na Mipangilio ya Miradi.
“Hakuna swali kuhusu hilo; tabaka la kati ndilo punda wa uchumi.”
“Tabaka la juu “limelindwa” kutokana na masaibu ya kiuchumi kupitia kuweka akiba, mishahara bora na wanaweza kubadilisha mifumo iwapendelee, kama malipo ya uzeeni na marupurupu. Matajiri wamekingwa kutokana na vilio vya maskini na tabaka la kati. Hilo linawafanya kukosa utu kirahisi. Maskini wanatumai siku moja kuwa katika tabaka la kati au matajiri, na pengine katika maisha yao,” anafafanua Profesa Iraki.
Mhadhiri wa Uchumi katika Chuo Kikuu cha Kenyatta, Profesa George Kosimbei, anafafanua sababu za tabaka la kati kuathiriwa ziadi na mikakati ya ushuru.
Profesa Kosimbei anahoji kuwa maskini wanaojumuisha tabaka la chini vilevile huathirika tabaka la kati linaposakamwa zaidi.