Makundi ya vijana yalemea gavana Sakaja huku yakitawala maeneo ya maegesho CBD
LICHA ya juhudi za mara kwa mara za maafisa wa Jiji la Nairobi kukomesha huduma haramu za vijana kusimamia maegesho katika barabara, wanaendelea bado vijana hao kuhangaisha madereva.
Vijana hao wamebadilisha baadhi ya barabara kama Banda, Kimathi na egesho la Sunken Car Park kuwa ngome zao, huku juhudi za kuwaondoa zikishindikana.
Vijana hawa huonekana wakielekeza magari katika nafasi za maegesho, wakati mwingine hata zisizo rasmi.
Wengine hukimbia mbele ya gari ili kuwaonyesha mahali pa kuegesha.
Hata hivyo, si wafanyakazi halali wa Kaunti ya Nairobi, bali ni kundi lisilo rasmi ambalo limejipenyeza na kutawala shughuli za maegesho katika eneo la kati la jiji (CBD).
Serikali ya kaunti imekiri kushindwa kudhibiti kundi hilo, hali inayosababisha kupoteza mapato kila mwaka.
Inadaiwa kuwa vijana hao wameunda mtandao haramu kwa kushirikiana na baadhi ya maafisa wasio waaminifu wa kaunti, wakigeuza barabara kuwa maeneo yao binafsi ya kujinufaisha.
Ingawa mfumo wa kulipia maegesho umewekwa kidijitali, fedha taslimu bado hutawala mchakato huo.
Madereva hulazimika kutoa fedha ili kupata nafasi au kuhakikisha magari yao yako salama.
Wanaokataa hutishiwa, na wakati mwingine magari yao huharibiwa.
Maegesho ni miongoni mwa vyanzo vikuu vya mapato kwa Kaunti ya Nairobi, pamoja na ushuru wa ardhi, leseni za biashara na matangazo.
Hata hivyo, pesa zinazokusanywa kutoka sekta hii zimekuwa zikipungua kila mwaka wa kifedha.
Katika miaka minne iliyopita, kaunti imekuwa ikipoteza angalau Sh1 bilioni kila mwaka kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo ushirikiano kati ya baadhi ya wahudumu wa maegesho na vijana hao.
Kwa mfano, mwaka wa kifedha uliomalizika Juni 2022, kaunti ililenga kukusanya Sh3 bilioni lakini ikapata Sh1.87 bilioni pekee.
Mwaka uliofuata, ilikusanya Sh1.86 bilioni, ikikosa kufikia lengo lake kwa zaidi ya Sh1 bilioni.
Hali kama hiyo ilijirudia mwaka wa 2024, ambapo Sh1.97 bilioni zilikusanywa zikipungua kwa Sh1.03 bilioni ambazo kaunti ililenga.
Afisa Mkuu wa Mapato wa Kaunti ya Nairobi, Tiras Njoroge, alisema kaunti hupoteza takriban Sh300,000 kila siku kutokana na shughuli za vijana hao kutawala maegesho, ambao wanakadiriwa kuwa zaidi ya 200.
Alionya kuwa kundi hilo pia ni tishio la usalama kwa madereva.
“Wakati mwingine wao huzidi hata wahudumu halali wa maegesho katika baadhi ya barabara,” alisema Njoroge, akiongeza kuwa vitendo vyao vinajumuisha vitisho, wizi na uharibifu wa magari ya wanaokataa kushirikiana nao.
Kwa mujibu wa sheria za kaunti, ni kosa kwa mtu yeyote kuelekeza au kusaidia kuingiza gari katika nafasi ya maegesho bila idhini.
Sheria pia zinakataza kuhifadhi nafasi au kuzuia utekelezaji wa kanuni za maegesho.
Aidha, magari yanayopatikana yameegeshwa bila kulipia yanaweza kufungwa au kuvutwa.
Hata hivyo, licha ya kuwepo kwa sheria hizo, utekelezaji wake umekuwa changamoto.
Mkurugenzi wa Mapato wa kaunti, John Ntoiti, alisema tatizo hilo limekita mizizi kiasi cha kufikia kiwango cha kutisha.
“Unawakamata lakini ndani ya dakika chache wanakuwa huru kwa sababu ya dhamana ndogo ya Sh1,000 au Sh2,000. Hali hii inawatia moyo kuendelea na shughuli zao,” alisema.
Aliongeza kuwa hata oparesheni za mara kwa mara hazijatoa suluhu ya kudumu, kwani vijana hao hurudi barabarani mara moja baada ya msako kukamilika.
Uchunguzi unaonyesha kuwa vijana hao hufanya kazi kwa vikundi vilivyo na viongozi wanaojulikana kama “Mwenyekiti”, na kila kundi hudhibiti eneo lake. Ni marufuku kwa mtu kufanya kazi katika eneo la kundi lingine bila ruhusa.
Baadhi yao hupata kati ya Sh1,500 na Sh2,500 kwa siku, kulingana na wingi wa kazi na aina ya huduma wanazotoa.
Wengine hushirikiana na walinzi wa majengo ili kupata nafasi zilizohifadhiwa, ambazo hupewa madereva kwa malipo ya ziada.
Cha kushangaza, baadhi ya madereva wamechangia kuenea kwa tabia hii kwa kuwaamini vijana hao kupita kiasi. Wapo wanaowaachia funguo za magari ili watafutiwe nafasi ya maegesho.
Hali hii inaonyesha jinsi mfumo wa maegesho katika Jiji la Nairobi ulivyotekwa na mitandao haramu, huku madereva wakiachwa mikononi mwa watu wanaonufaika na udhaifu wa usimamizi wa kaunti.