Mama taabani akidaiwa kuuza bintiye kwa raia kutoka Ujerumani
MAMA mmoja mjini Mombasa anachunguzwa kwa madai alitumia bintiye wa miaka 16 kama kitega uchumi kwa kumuuza kwa raia wa Ujerumani.
Wapelelezi kutoka Kitengo cha Kupambana na Ulanguzi wa Binadamu na Ulinzi wa Watoto wameanza kuchunguza rekodi za simu za mkononi ili kufuatilia fedha alizopokea kutoka kwa mtalii huyo Mjerumani .
Raia huyo wa Ujerumani, Traumer Reinhard, tayari ameshtakiwa kwa makosa kadhaa kama vile kunajisi mtoto na ulanguzi wa binadamu.
Wachunguzi sasa wanaelekeza uchunguzi wao kwa mwanamke huyo anayeshukiwa kuwezesha uhalifu huo kwa madai kwamba alitumia stakabadhi za kitambulisho za dada mkubwa wa msichana huyo kumuonyesha kama mtu mzima kabla ya kumkabidhi kwa mgeni huyo.
Stakabadhi zilizowasilishwa katika Mahakama ya Shanzu zinaonyesha mzazi, ambaye anatarajiwa kumlinda mtoto wake, anadaiwa kushiriki katika kitendo hicho.
Kwa mujibu wa hati ya kiapo iliyowasilishwa na Sajenti Wycliffe Jefwa, afisa wa Idara ya Upelelezi wa Jinai katika Kitengo cha Kupambana na Ulanguzi wa Binadamu na Ulinzi wa Watoto, Reinhard alikamatwa Februari 24 katika nyumba ya ghorofa iliyoko Nyali, Kaunti ya Mombasa.
Alipelekwa mahakamani mnamo Februari 27, 2026 kwa ajili ya kusomewa mashtaka ya kumnajisi mtoto, lakini hati ya mashtaka ilifanyiwa marekebisho Machi 2 ili kujumuisha shtaka la ulanguzi wa binadamu.
Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma iliagiza kwamba uchunguzi huo uhamishwe kutoka Kitengo cha Polisi wa Watalii cha Bamburi, ambako ulianza kushughulikiwa, hadi Kitengo cha Kupambana na Ulanguzi wa Binadamu na Ulinzi wa Watoto Idara ya Upelelezi wa Jinai.
Uchunguzi huo sasa umepanuliwa na kumhusisha mama wa mtoto huyo, anayetajwa katika stakabadhi za mahakama kama C.W, ambaye alikamatwa kwa madai kwamba alipokea malipo kutoka kwa mshukiwa huyo Mjerumani.
Hata hivyo, mwanamke huyo aliachiliwa kwa dhamana katika kituo cha polisi ili kuwapa wapelelezi muda wa kukamilisha uchunguzi.