Habari

Maraga sasa ataka arejeshewe walinzi

Na CHARLES WASONGA June 27th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

JAJI Mkuu Mstaafu David Maraga ameitaka serikali imrejeshee walinzi wake waliondolewa Alhamisi baada ya kuungana na waandamanaji jijini Nairobi Jumatano.

Kwenye barua kwa Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen na Inspekta Jenerali wa Polisi, Bw Maraga alitaja hatua hiyo kama haramu.

“Mnamo Juni 25, 2025 jioni afisa mmoja aliagizwa kurejesha silaha yake. Siku iliyofuata, niliarifiwa kuwa maafisa wengine wa usalama waliagizwa kuondoka na waripoti katika vituo vyao, bila kupewa maelezo zaidi,” Bw Maraga akaongeza.

Alieleza kuwa ni haki yake ya kikatiba kama Jaji Mkuu mstaafu kupewa ulinzi kulingana na kanuni iliyowekwa katika Sheria kuhusu Malipo ya Pensheni kwa Naibu Rais na Maafisa Wakuu wa Serikali.

“Ningependa kukumbusha uogozi wa Huduma ya Kitaifa ya Polisi na Wizara ya Usalama wa Ndani kwamba Katiba ya sasa imenihakikisha ulinzi ninaopasa kupewa kila wakati. Ni kwa msingi huu ambapo nataka nirejeshewe walinzi,” Bw Maraga akaongeza.

Jaji huyo Mstaafu ambaye ametangaza azma ya kuwania urais katika uchaguzi mkuu wa 2027, alikariri kuwa hatua ya kuondolewa kwa walinzi wake ni haramu kisheria na kunahatarisha usalama wake.

Wakati huo huo, wabunge sasa wanaitaka serikali kusitisha ulipaji wa pensheni kwa Bw Maraga, Makamu wa Rais wa zamani Kalonzo Musyoka na Spoka wa zamani Justin Muturi kwa kushiriki katika maandamano ya kuipinga.

Wakichangia mjadala kuhusu hoja ya kujadili maafa na uharibifu uliotokea katika maandamano ya Jumatano, wabunge wa mrengo wa serikali walisema watatu hao wamekiuka matakwa ya Sheria kuhusu Malipo ya Pensheni ya Naibu Rais na Maafisa Wakuu wa Serikali.

Wakiongozwa na kiongozi wa wengi Naibu Spika Glady Boss Shollei wabunge hao Alhamisi walisema sheria hiyo inawahitaji Maafisa Wakuu waliostaafu kutoshiriki siasa.

Bi Shollei ambaye ni Mbunge Mwakilishi wa Kike wa Uasin Gishu alisema serikali haiwezi kuendelea kuwalipa pensheni watu ambao wanaendelea kuwapotosha vijana kwa kuwashawishi kushiriki maandamano na kusababisha machafuko nchini.

“Aibu kwako Jaji Mkuu Maraga. Wakati huu unalipwa pensheni na serikali, inagharamia magari yako, wapishi wako na watumishi wengi kisha unajitokeza barabara kushiriki maandamano na kupotosha watoto wetu waharibu mali ya watu wengine. Hilo halitawezekana na sharti malipo hayo yasitishwe,” Bi Shollei akasema.

Wengine waliounga mkono wazo hilo ni: Silvanus Osoro (Mugirango Kusini), Farah Maalim (Dadaab) na Benjamin Lagat (Ainamoi).