Habari

Mashirika ya misaada na mishenari yafunga virago Bonde la Kerio

Na BARNABAS BII June 2nd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MASHIRIKA ya kutoa misaada pamoja na Kanisa Katoliki yameanza kujiondoa kwenye ukanda wa Bonde la Kerio, Elgeyo-Marakwet  kutokana na utovu wa usalama uliosababishwa na majangili waliojihami. 

Majangili hao wamekuwa wakiwalenga wafanyakazi wa mashirika hayo ya kutoa misaada.

Kwa muda wa miezi miwili iliyopita, kumekuwa na mauaji ya watu wasio wazawa na sasa mashirika hayo pamoja na kanisa Katoliki yamesitisha kabisa shughuli zao.

Kundi la Kimisheni ya Benedictine Sisters ni kanisa katoliki la hivi punde kusitisha shughuli zake za kutoa msaada ukanda wa Kerio.

Hii ni kwa sababu wafanyakazi wao sasa wanahofia kuendelea na kazi kwenye ukanda huo kutokana na usalama wao.

Hii ni kufuatia mauaji ya Kasisi Allois Cheruiyot Bett wa Kanisa la Mathias Mulumba na dayosisi ya Tot mnamo Alhamisi wiki jana.

Pia kumekuwa na kampeni inayowalenga watu ambao si wazawa wa Bonde la Kerio hali hiyo ikisababisha watumishi wa umma hasa walimu kuhepa eneo hilo.

“Kutokana na taharuki ambayo imekuwa ikishuhudiwa, tumeafikia uamuzi wa kufunga misheni yetu kabisa hadi eneo hilo liwe salama kwa utoaji wa huduma,” ikasema taarifa kutoka Mtawa Rosa Pascal.

Alisema utovu wa usalama unaoendelea kushuhudiwa, umechangia matatizo ya kisaikolijia na kihisia miongoni mwa watawa pamoja na wafanyakazi wao kutoweza kutoroka na kushindwa kuendelea kutoa huduma.

“Hatua ambayo tumeichukua inalenga kuhakikisha usalama wa watawa wanaofanya kazi eneo hilo, wafanyakazi wetu na wale ambao hutembelea misheni yetu kupokea huduma mbalimbali,

“Pia tunalenga kushinikiza serikali ipate suluhu kwa amani ya kudumu kwa kutwaa silaha haramu mikononi mwa majangili,” akaongeza Mtawa Rosa.

“Pia inalenga kuwakumbusha wanaoishi ukanda wa Bonde la Kerio umuhimu wetu kwa jamii. Iwapo jamii inaona huduma ambazo zinatolewa na misheni yetu si muhimu kwao basi hakuna haja ya kuwa hapa,” akasema.

Maaskofu wametoa wito kwa uchunguzi wa ndani kuhusiana na mauaji ya Kasisi Allois wa Dayosisi ya Eldoret na James Maina wa Nyahururu, wakisikitikia kuwapoteza watumishi waaminifu wa Mungu.