Maswali kuhusu fedha za ushuru wa nyumba ‘kuhamishwa’ kujenga masoko
UKOSEFU wa uwazi katika Sheria ya Nyumba za Bei Nafuu umeruhusu serikali inayoongozwa na William Ruto kuhamisha fedha zilizokusudiwa kujenga nyumba za bei nafuu kufadhili miradi mingine kama masoko kote nchini.
Wiki hii, Rais Ruto alizua mjadala mkali kuhusu uwezekano wa matumizi mabaya ya fedha zinazokusanywa kila mwezi kupitia ushuru wa nyumba nafuu, akisema kwamba pesa hizo pia zinatumika kukamilisha ujenzi wa masoko ambayo baadhi yake yalianzishwa enzi za utawala wa Mwai Kibaki, na hayahusiani na mradi wa nyumba hizo.
“Hatutumii tu ushuru huo kujenga nyumba za bei nafuu. Tunautumia kujenga masoko pia,” alisema Dkt Ruto.
“Sasa tuna masoko 260 yanayoendelea kujengwa nchini. Tuna mabweni ambayo karibu yaanze kujengwa. Hivyo basi, vijana wetu walio vyuoni watanufaika. Akina mama wetu na wafanyabiashara masokoni watanufaika pia,” aliongeza.
Sheria ya Nyumba Nafuu inaweka ushuru wa asilimia 1.5 ya mshahara wa mfanyakazi, na mwajiri anatakiwa kuchangia kiwango sawa.
Wafanyabiashara wa kujitegemea wanatozwa asilimia 1.5 ya mapato yao ikiwemo faida kutoka kwa biashara au pensheni.
Mbali na nyumba za bei nafuu na miundombinu yake, sheria hiyo inaruhusu Bodi ya Nyumba Nafuu kutumia fedha hizo kujenga nyumba za taasisi kama vile mabweni na makazi ya watumishi wa umma.
Serikali ya Kenya Kwanza ya Dkt Ruto inapanga kukusanya takriban Sh500 bilioni kutokana na ushuru huo wa asilimia 1.5 unaolipwa na Wakenya, hasa wafanyakazi waajiriwa ambao waajiri wao huchangia kiasi sawa ili kujenga nyumba na miundombinu ya kijamii na huduma nyingine za umma.
John Denge, mtaalamu wa masuala ya mali isiyohamishika, anaeleza kuwa kuna pengo katika sheria hiyo linaloruhusu serikali kuelekeza fedha hizo kwenye miundombinu ya kijamii isiyohusiana moja kwa moja na miradi ya nyumba, hasa kutokana na kasi ndogo ya matumizi ya fedha hizo.
“Sheria haisemi wazi kama ‘miundombinu husika’ inapaswa kuwa ndani ya mradi. Inatoa nafasi kubwa ya kuelekeza fedha kwenye masoko yanayoendelea kujengwa,” alisema Denge.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Nyumba Nafuu, Sheila Waweru, alisema sheria hiyo haizuii matumizi ya fedha hizo kwenye miundombinu ya kijamii tu ndani ya mradi.