Habari

Mataifa ya Afrika yalalamikia vikwazo vipya vya Rais Trump

Na HILARY KIMUYU June 6th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

TUME ya Umoja wa Afrika (AUC) imelalamikia vikwazo vya hivi punde vya usafiri vilivyowekwa na Amerika dhidi ya raia wa mataifa mbalimbali, wakiwemo raia kutoka baadhi ya mataifa ya Afrika.

Kwenye taarifa iliyotolewa jana, tume hiyo ilitambua haki ya Amerika ya kulinda mipaka yake lakini ikaitaka nchini kutekeleza hatua za kufanikisha hilo katika hali ambayo haiathiri uhusiano wake na Afrika.

Vikwazo hivyo, vilivyotiwa saini na Rais Donald Trump, vinawazima kabisa raia kutoka nchini 12 kuingia Amerika.

Aidha, hatua hiyo imeongeza muda wa utekelezwa vikwazo vilivyowekewa raia wengine kutoka nchi saba.

Nchi kadhaa za Afrika ni miongoni mwa zile zilizoathirika, hali ambayo imeibua taharuki katika bara hili.

“Tume inaelezea hofu kuhusu madhara ya hatua kama hiyo ya kuwekewa watu fulani vikwazo vya usafiri. Hatua hiyo itaathiri mahusiano ya raia wa Amerika na wale wa mataifa husika Afrika, mahusiano katika nyanja za masomo na mahusiano mapana ya kibiashara ambayo yamekuzwa kwa miongo mingi,” taarifa hiyo kutoka AUC ikasema.

Tume hiyo ilikariri umuhimu wa upaliliaji wa mahusiano ya karibu kati ya Afrika na Amerika katika kudumisha amani, ustawi na ushirikiano wa kimataifa.

AUC ilitoa wito kwa serikali ya Amerika kukumbatia mtindo wa mashauriano ambayo ni wazi kati yake na nchi zilizoathirika.

“Tume hii iko tayari kuunga mkono juhudi zinazoendeleza uelewa, kusuluhishwa kwa tofauti na uimarishaji wa ushirikiano kati ya Afrika na Amerika,” taarifa hiyo ikaongeza.

Mafuruku iliyotangazwa na Rais Trump Jumatano usiku itaanza kutekelezwa mnamo Jumatano, Juni 9.

Ni mojawapo ya hatua kali za aina yake ambayo Rais Trump amechukua katika muhula wake wa pili afisini.