Mauaji yatishia ndoa ya ODM na UDA
KUENDELEA kwa utekaji nyara, kutoweshwa kwa nguvu na mauaji ya kiholela kunatishia makubaliano ya kisiasa kati ya Rais William Ruto na Waziri Mkuu wa zamani Raila Odinga.
Viongozi kutoka upinzani na hasa vijana kutoka Luo Nyanza wanawekea presha serikali ya Rais Ruto kufafanua ni nani anayehusika na utekaji wa wapinzani wa serikali na kukomesha mara moja ukatili huu ambao unaweza kuleta mgawanyiko katika serikali Jumuishi.
Baadhi ya wanachama wa chama ODM wamesema vifo vya kutatanisha vilikuwa miongoni mwa mambo ambayo viongozi hao wawili walikubaliana kuvishughulikia katika makubaliano yao.
Katika makubaliano ya vipengele 10 yaliyotiwa saini mwezi Machi ambayo yalisababisha kuundwa kwa Serikali Jumuishi, viongozi hao walikubaliana kushirikiana, kuendeleza umoja na kusukuma mbele ajenda ya kijamii na kiuchumi ya Kenya.
Tayari, viongozi waliokuwa wakishabikia ushirikiano mpya kati ya Dkt Ruto na Bw Odinga na kusifu maendeleo katika maeneo ambayo awali yalitengwa, sasa wameanza kulaumu washirika wao wa kisiasa, wakitishia kuchukua hatua ambazo hawakutaja iwapo maovu haya yataendelea.
Wito huu umeongezeka kufuatia kifo cha kutatanisha cha Albert Ojwang mwalimu na mwanablogu wa Voi akiwa korokoroni, tukio ambalo limezua hasira kote nchini.
Ojwang aliripotiwa kufariki Jumapili asubuhi katika hali isiyoeleweka, jambo lililosababisha lawama kali.
Polisi wanadai alijiua kwa kujigonga kichwani kwenye ukuta wa seli yake katika Kituo Polisi cha Central Nairobi lakini ripoti ya upasuaji wa mwili ilionyesha alishambuliwa.
Jana, Bw Odinga alilaani kifo cha Ojwang mikononi mwa polisi akisema visa kama hivyo vinaweza kufanya nchi kuporomoka.
“Ikiwa wananchi hawawezi kutofautisha kati ya aina mbili za ukosefu wa haki – ukatili wa polisi na kuuawa na umati – basi tunakabiliwa na hatari ya kufeli kama taifa,” aliongeza.
Waziri Mkuu wa zamani alitoa wito kwa Huduma ya Kitaifa ya Polisi kuchukua hatua za haraka na za dhati, akisisitiza kwamba uwajibikaji si chaguo.
Huku umma, viongozi na wanaharakati wa haki za binadamu wakitaka haki itendeke, kauli kutoka kwa viongozi wa ODM yanaashiria uwezekano wa ufa katika serikali jumuishi.
Katika taarifa zao, baadhi ya wabunge wa ODM, walisema kwamba katika wiki na miezi ya hivi karibuni, kumekuwa na ongezeko la visa vya utekaji, kupotea kwa watu, na vifo vinavyotokea mikononi mwa watu wanaoshukiwa kuwa maafisa wa polisi.
Rais Ruto alikuwa ameahidi kukomesha utekaji nyara, lakini maovu hayo bado yanaendelea kushuhudiwa kote nchini.
Dkt James Nyikal, Mbunge wa Seme, aliyesoma taarifa kwa niaba ya Wabunge 14 wa ODM, alisema hakuna mtu aliye na haki ya kumkamata au kumuua mtu kwa sababu tu ya kutokubaliana na maoni yake.
“Kifo cha Albert Ojwang kisiwe sehemu ya takwimu za vijana waliouawa bure. Lazima uchunguzi ufanywe na waliohusika washtakiwe haraka. Maafisa wausalama lazima wawajibishwe,” alisema.
Mbunge huyo wa Seme alimtaka Rais kuchukua usukani, arejeshe nidhamu katika maafisa wa usalama na kudhibiti vitendo vya kiholela vya watu wenye mamlaka walioko karibu naye ambao wanajaribu kuwanyamazisha wananchi kwa mabavu.
Alisema kuwa taifa lisiloruhusu vijana wake kueleza maoni yao au kuuliza maswali ni taifa lililokufa.
Millie Odhiambo, Mbunge wa Suba North, alimshauri Rais achukue hatua dhidi ya waliohusika na utekaji na mauaji hayo.
“Katika makubaliano yetu, hakuna ushirikiano kuhusu ukosefu wa uvumilivu, au kukandamiza haki za binadamu. Huo si msimamo wa chama chetu. Hatuwezi kusaliti maadili yetu kama chama. Tumemweleza Rais kuhusu suala hili na aliahidi kuwawajibisha maafisa wake waliopoteza mwelekeo,” alisema Bi Odhiambo, ambaye pia ni Kiranja wa Wachache katika Bunge la Taifa.
Bw Kasmuel Mcoure, mwanachama wa vijana wa ODM, alisema utekaji nyara haukuwa sehemu ya makubaliano yao na Ruto.
“Tunataka kujua kilichotokea kwa Albert Ojwang kutoka Mawego hadi Nairobi. Kama wanachama wa ODM Youth League, tunamwambia Ruto kuwa kama makubaliano yetu yanajumuisha kuua watu wetu, basi hatutaki huo mkataba,” alisema Mcoure.
Aliongeza: “Ni ODM iliyosafisha jina la Rais. Kama makubaliano ya ODM–UDA yanamaanisha watu wetu wanapewa hela ndogo huku watoto wetu wakiuawa, basi hatuwezi kuwa sehemu yake.”
Alisema iwapo hawatapokea majibu wanayotafuta na haki kwa Ojwang, watarejea mitaani na kuandamana dhidi ya serikali ya Rais Ruto.
Akizungumza katika mahojiano kwenye kipindi cha Fixing the Nation cha Nation FM, Waziri wa Kawi Bw Opiyo Wandayi, alielezea masikitiko yake kuhusu tukio hilo lakini akaomba utulivu huku uchunguzi ukiendelea.
Sio mara ya kwanza kwa viongozi wa ODM kutishia kuvunja makubaliano hayo.
Wakati Mbunge wa Kasipul, Charles Ong’ondo Were, aliuawa, Mwenyekiti wa Kitaifa wa ODM, Gladys Wanga, alisema kwamba upinzani ulikubali kushirikiana na serikali lakini haimaanishi wanachama wao wateswe au kuumizwa.