Mawakili wa Lissu walalamika katika Umoja wa Mataifa
MAWAKILI wa kiongozi wa upinzani wa Tanzania aliye kizuizini, Tundu Lissu, Ijumaa waliwasilisha malalamishi kwa Jopokazi la Umoja wa Mataifa kuhusu Kuzuiliwa Kinyume cha Sheria, katika juhudi za kuongeza shinikizo la kimataifa aachiliwe.
Lissu, ambaye ni mwenyekiti wa chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania na aliyekuwa wa pili katika uchaguzi wa urais wa mwaka 2020, alikamatwa mwezi uliopita na kushtakiwa kwa kosa la uhaini ambalo adhabu yake ni kifo, kutokana na kauli anazodaiwa kutoa akiwarai wafuasi wake kuzuia uchaguzi mkuu wa Oktoba kufanyika.
Msemaji wa serikali ya Tanzania hakujibu mara moja ombi la kutoa maoni kuhusu suala hilo.
Ingawa Rais Samia Suluhu Hassan amesifiwa kwa kulegeza ukandamizaji wa kisiasa, anakabiliwa na maswali kuhusu utekaji nyara usioeleweka wa wakosoaji wa serikali katika miezi ya hivi karibuni.
Hassan, ambaye atagombea tena urais mwezi Oktoba, amesema serikali yake inaheshimu haki za binadamu na ameagiza kufanyika kwa uchunguzi kuhusu matukio hayo ya utekaji nyara.
Wakili w kimataifa wa Lissu, Robert Amsterdam, alisema malalamishi yaliyowasilishwa kwa jopokazi la Umoja wa Mataifa, ambalo hutoa maoni lakini halina mamlaka ya utekelezaji, ni sehemu ya kampeni kubwa ya kushinikiza kuachiliwa kwa Lissu.
Bunge la Ulaya mwezi huu lilipitisha azimio lililolaani kukamatwa kwa Lissu na Amsterdam alisema ataomba Wizara ya Masuala ya Kigeni ya Amerika kuwekea vikwazo maafisa wa utawala wa Rais Hassan.
“Kuanzia waendesha mashtaka, majaji, polisi, wote waliohusika katika kesi hii ya mashtaka ya uongo wanapaswa kufahamu kuwa wanapaswa kulinda mali yao iliyoko Amerika,” Amsterdam aliiambia Reuters.
Katika kujibu azimio la Bunge la Ulaya, wizara ya masuala ya nje ya Tanzania ilisema shutuma kutoka nje kuhusu kesi hiyo zinategemea “taarifa zisizo kamili au zenye upendeleo.”
Wizara ya Masuala ya Nje ya Amerika haikujibu mara moja ombi la kutoa maoni.
Lissu, ambaye alipigwa risasi mara 16 katika shambulio la mwaka 2017 ambalo hakuna mtu aliyewahi kushtakiwa, atafikishwa mahakamani Jumatatu.
Kabla ya kufikishwa mahakamani wiki iliyopita, serikali ya Tanzania iliwakamata wanaharakati wa haki za binadamu kutoka Kenya na Uganda walioenda kushuhudia kesi hiyo.