Habari

Mbarire alipukia Gachagua kwa kumhangaisha kisiasa

Na GEORGE MUNENE June 28th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

GAVANA wa Embu Cecily Mbarire amemshutumu vikali aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua kwa kumhangaisha na kumdhalilisha kisiasa akimtaka aepuke kaunti hiyo.

Bi Mbarire amesema kuwa hamwogopi Bw Gachagua na atamkabili peupe iwapo ataendelea kumpiga vita kisiasa.
“Rigathi Gachagua aje Embu tena. Alikuja hapa na kuniita msaliti kisha akanitisha kuhusu msimamo wangu wa kisiasa, sitanyamaza tena,” akasema Bi Mbarire akiwa mwenye hamaki tele katika makao makuu ya kaunti.
“Sijali kuhusu nguvu zako za kisiasa lakini hutaendelea kunitishia na kunihangaisha. Sitanyamaza na kama wewe ni Mungu, yachukue maisha yangu,” akaongeza.
Gavana huyo alidai kuwa ghasia za kisiasa ambazo zimekuwa zikishuhudiwa Embu zinatokana na uchochezi wa aliyekuwa naibu rais huku akisema hatakubali matukio kama hayo tena.
“Kibaya zaidi ambacho kinaweza kunitendekea ni nife na nitakufa mara moja. Huwezi kugeuza Embu uwanja wa vita wala huwezi kudai unapenda Embu kisha wakati huo huo unawaadhibu,” akasema.
Kiongozi huyo alidai Bw Gachagua anapanga kuchukua mamlaka kupitia mlango wa nyuma huku akidai kuwa kuna mwanasiasa mmoja mashuhuri Embu ambaye anatumiwa na aliyekuwa naibu rais kuvuruga utawala wake.
“Mwanasiasa huyo ni mtu wake wa mkono lakini anaharibu taaluma yake. Hata watu ambao walitekeleza uharibifu hapa ni watu ambao walisafirishwa kutoka nje ya Embu,” akasema.
Kiongozi huyo alisema maandamano yameonyesha kuwa si suala la Gen Z kupigania haki zao bali wanasiasa sasa wameingilia ndani na kudhamini makundi ya waporaji ili kuwalenga wapinzani wao wa kisiasa.
Bi Mbarire alidai magenge yaliyokodishwa wakati wa maandamano hayo yalilenga mbunge wa Mbeere Kusini Nabert Kariuki ambaye hoteli yake ilivamiwa na kuporwa na kulikuwa na jaribio la kuvamia makazi yake mashinani.
Aliahidi kuwa sasa atakabiliana na wapinzani wake ambao wamekuwa wakipanga fujo na maasi Embu huku akisisitiza hatajiunga na mrengo wa Bw Gachagua.

Bi Mbarire amekuwa akikabiliwa na shinikizo kali za kisiasa huku Bw Gachagua na aliyekuwa Waziri wa Utumishi wa Umma Justin Muturi wakivumisha wimbi la upinzani Embu.

Mwezi uliopita, Gavana huyo alidai kuwa alikuwa kuna baadhi ya maafisa wa ngazi ya juu serikali ambao walikuwa wakimdharau katika siasa za Embu na wanazuru kaunti hiyo bila kumfahamisha.

Matamshi hayo yalionekana kumlenga Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki lakini baadaye wawili hao walikutana na kuzika tofauti zao.