Habari

Mbunge ashtakiwa kwa kuweka picha kwenye mabango

Na SAM KIPLAGAT June 21st, 2025 Kusoma ni dakika: 1

WAKILI mmoja jijini Nairobi amemshtaki Mbunge wa Kajiado Kaskazini, Onesmus Ngogoyo, akimlaumu kwa kukiuka sheria kwa kuweka jina na picha yake kwenye mabango ya miradi inayofadhiliwa na serikali kupitia Hazina ya Serikali ya Kitaifa ya Maendeleo ya Maeneobunge (NG-CDF).

Wakili huyo, Shadrack Wambui, anasema kuwa hatua hiyo ni kinyume na maadili ya uongozi na uadilifu, na anamtaka mbunge huyo aondoe mabango yote yenye jina lake, picha, na kauli mbiu za kisiasa kwenye shule, barabara, na miundombinu mingine ya umma katika eneo lake.

Katika kesi hiyo iliyowasilishwa katika Mahakama Kuu mbele ya Jaji Christine Meoli, Bw Wambui anasema kuwa mbunge huyo amekuwa akijinufaisha kisiasa kwa kutumia miradi ya umma, baadhi ikiwa ilitekelezwa kabla ya kuchaguliwa kwake.

“Mbunge huyo ameweka jina na picha yake kwenye karibu kila mradi wa maendeleo wa serikali ndani ya eneo lake, na katika hali nyingi, picha na jina lake vinachukua nafasi kubwa kupita kiasi kwenye mabango, hivyo kufunika taarifa muhimu kwa wananchi,” alisema wakili huyo.

Bw Wambui anasema kuwa tabia hiyo inakandamiza ukweli na hutoa taswira ya kupotosha, ikiwafanya wananchi kuamini kimakosa kwamba wabunge ndio wanaotekeleza miradi kama barabara, shule, na vituo vya afya.

Seneti ya Kenya, katika ripoti ya Mei 21, 2025, ilikemea vikali tabia hiyo na kuwataka maafisa wa umma kuzingatia maadili katika utekelezaji wa majukumu yao ya umma. Pia ilizitaka Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) na Mdhibiti wa Bajeti kuchukua hatua madhubuti za kudhibiti tabia hiyo. Kesi hiyo itatajwa Julai 22, 2025.