Mchungaji akiri alishindwa kupatanisha muumini aliyeuawa katika mzozo wa ndoa
MCHUNGAJI kutoka Kanisa la New Life International amesimulia mbele ya mahakama mjini Eldoret jinsi juhudi zake za kusuluhisha mzozo wa wanandoa waliotengana ziligonga mwamba na hatimaye kupelekea mume kumuua mkewe.
Mchungaji Timothy Kizili, anayejulikana pia kama ‘Favour’, alitoa ushahidi Jumatano katika kesi ya mauaji ambapo Francis Mwangi Ndirangu anashtakiwa kwa kumuua mkewe Rael Cherop Biwott.
Marehemu alikuwa mhasibu katika Hospitali ya Mafunzo na Rufaa ya Moi mjini Eldoret.
Kanisa la New Life International linaloongozwa na mhubiri wa Ezekiel Odero linahimiza upatanisho wa wanandoa waliotengana na kurejesha ndoa zilizovunjika. Hata hivyo, kulingana na mchungaji huyo wa Eldoret, kadri alivyozidi kuwashauri wanandoa hao, ndivyo uhusiano wao ulivyozidi kuwa sumu.
Bi Biwott, 44, aliripotiwa kutoweka mnamo Juni 23, 2024, na viungo vya mwili wake vilipatikana sehemu mbalimbali katika kaunti za Uasin Gishu na Nandi kati ya Juni 24 na Juni 27.
Ingawa Ndirangu alidai kwa polisi kuwa walichukua matatu kuelekea nyumbani, picha za CCTV baadaye zilionyesha kuwa waliondoka kwa gari aina ya Toyota Succeed ambalo alikuwa amekodisha.
Mchana wa Juni 24, baadhi ya viungo vya mwili wa marehemu vilipatikana vikiwa vimefungwa ndani ya gunia kando ya barabara katika kijiji cha Kapsilegaa, Motwot, Kaunti ya Nandi. Viungo hivyo vilijumuisha miguu na viungo vya ndani vilivyokuwa vimefungwa ndani ya mfuko wa plastiki.
Mauaji hayo yaliendelea kutisha zaidi pale sehemu nyingine za mwili wake kikiwemo kichwa na mikono zilipopatikana zimetupwa barabarani katika kijiji cha Lamaiyat, Kaunti ya Uasin Gishu, siku hiyo hiyo.
Haikuwa hadi saa 12:40 jioni siku hiyo ambapo Bw Ndirangu aliripoti kupotea kwa mkewe katika Kituo cha Polisi cha Eldoret Central.
Uchunguzi wa maiti uliofanywa katika Hospitali ya Mafunzo na Rufaa ya Moi mbele ya familia ya marehemu na mawakili, ulibaini kuwa Bi Biwott alipata majeraha mabaya ya shingo na ya kichwa kutokana na kupigwa kwa nguvu.
Kwa mujibu wa mchungaji, marehemu alijiunga na kanisa lake miaka miwili iliyopita akitoka Kanisa la Deliverance. Kufikia wakati huo, wanandoa hao waliokuwa wakiishi katika mtaa wa Shauri, pembezoni mwa Eldoret, walikuwa tayari wanapitia changamoto kubwa za ndoa.
Alisema Bi Biwott alimwendea kutafuta ushauri wa ndoa baada ya kumweleza masaibu aliyokuwa akipitia. Wakati wa vikao hivyo, alimweleza kuwa maisha yake yalikuwa hatarini kutokana na vitisho vya mara kwa mara kutoka kwa mumewe.
“Marehemu alikiri kuwa alikuwa kwenye ndoa yenye sumu na kwamba mumewe alikuwa akimtishia maisha,” Mchungaji Kizili aliambia mahakama.
Aliongeza kuwa vikao vya ushauri vilifanyika bila mumewe, ambaye alihudhuria ibada moja tu ya kanisa pamoja na mkewe na watoto wao watatu.
“Hadithi yake ilikuwa ya kuhuzunisha. Nilijitahidi kuwashauri kwa matumaini ya kuwaunganisha tena ili waweze kuishi kwa amani na kufurahia ndoa yao,” alisema.
Kesi inaendelea kusikizwa…