Mchuuzi aliyepigwa risasi na polisi angali mahututi hospitalini, familia yasema
FAMILIA ya Boniface Kariuki, mchuuzi wa barakoa aliyepigwa risasi kichwani na afisa wa polisi wakati wa maandamano Jumanne, inasema angali mahututi na maisha yake bado yamo hatarini.
Hali yake haijabadilika hata baada ya upasuaji wa pili uliofanywa Alhamisi jioni, jambo ambalo limezidisha hofu miongoni mwa familia yake.
Kufikia Jumamosi alasiri, Kariuki hakuwa akizungumza isipokuwa maumivu, kulingana na msemaji wa familia, Bi Emily Wanjira.
“Tulimuona, hali yake ni mbaya sana. Hawezi kuzungumza, haoni, ana maumivu,” alisema Bi Wanjira kwa huzuni.
Bi Wanjira alisema huenda maisha ya kijana huyo hayatakuwa ya kawaida tena.
“Katika siku tatu zilizopita, siku mbili za kwanza alikuwa katika hatari mno. Ijumaa kulikuwa na mabadiliko kidogo, lakini sasa, Boniface hawezi kuzungumza na hatutarajii maisha yake kurudi kawaida,” aliongeza.
Mnamo Alhamisi jioni, madaktari katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH) walimfanyia upasuaji wa pili kujaribu kudhibiti uvimbe uliogunduliwa upande wa kushoto wa ubongo wake.
Licha ya hayo, familia inaendelea kuwa na matumaini japo mtoto wao yuko kwenye mashine ya kumsaidia kuwa hai.
“Boniface bado yuko ICU chini ya uangalizi mkali. Tunachojua ni kuwa, bado maisha yake yamo hatarini,” alisema Bi Wanjira.
Kwa mujibu wa wakili wa familia, Bw Lucas Murage, serikali imenyima familia hiyo msaada na kuiacha iking’ang’ana kulipa bili ya hospitali ambayo sasa imevuka Sh1milioni.
Familia hiyo imeeleza masikitiko yao kwa taasisi za serikali kama IPOA na Huduma ya Polisi ya Kitaifa kwa kutowajali licha ya tukio hilo kunaswa kwa video, iliyoonyesha Boniface akipigwa risasi.
“Hadi sasa, hakuna mtu yeyote kutoka serikali aliyewasiliana nasi,” alisema Bi Wanjira.