Habari

Mfanyakazi wa Mega Shopping Mall ashtakiwa kuiba Sh296 milioni ndani ya miaka saba

January 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MFANYAKAZI katika duka la jumla ameshtakiwa kuiba Sh296 milioni katika muda wa miaka saba kati ya 2018 na 2025.

Mohamed Osman Abdille ambaye pia anamiliki kampuni ijulikanayo kwa jina Fatzam Enterprises Limited (FEL) anadaiwa na kiongozi wa mashtaka ya umma (DPP) kwamba alificha kabisa kule alikopata pesa hizo.

Mahakama imeelezwa na DPP kwamba Abdille anayeshtakiwa pamoja na FEL alikuwa ameweka pesa hizo kwenye akaunti za Benki za Kenya Commercial Bank (KCB), Absa Bank na Equity Bank Limited (EBL) matawi ya Eastleigh Kaunti ya Nairobi.

Mshtakiwa, mahakama iliambiwa alikataa kufichua alikotoa zaidi ya Sh116 milioni ambazo polisi walikuta kwenye akaunti zake katika benki za KCB, Absa na EBL.

Pia mshtakiwa alikataa kata kata kwamba Sh107 milioni alizokuwa nazo zilikuwa zimepatikana kwa njia isiyo halali.

Alikana alijua pesa alizokuwa ameweka katika akaunti za benki hizo zilikuwa sehemu ya Sh296,069,084 zilizoibwa kutoka kwa Bw Abid Mohamed Ali kati ya Januari 1, 2018 na Feburuari 19, 2025.

Mahakama ilielezwa kwamba wakurugenzi wawili wa FEL-Mabw Abdille na Hussein Ibrahim Barre ambaye hakufika kortini kujibu mashtaka walificha kabisa kule pesa hizo zilitoka kwa kuagiza tambi (spaghetti) za mamilioni ya pesa kutoka kampuni ya Arabian Milling & Food Company.

Mbinu nyingine ambazo Abdille, Barre na FEL wanadaiwa walitumia kuficha pesa ni kuzihamisha na kuweka katika akaunti za kampuni ya Gigi International Limited, Marray and Sons Venture Limited, Arabian Milling & Food Company, Ada Food Gida Sanayive Tlc, Ismail Mohamed Ali na Hussein Ibrahim Barre.

Bw Abdille alikabiliwa na mashtaka 30 ya kula njama za kutekeleza uhalifu, wizi, kuficha alikotoa pesa na kuzihamisha kutoka akaunti ya FEL hadi kwa akaunti nyingine.

Upande wa mashtaka ulieleza mahakama kwamba Abdille aliiba Sh296,069,084 kati ya Januari 1, 2018 na Septemba 30, 2024.

Abdille anadaiwa alitekeleza uhalifu huo pamoja na FEL.

Mshtakiwa alidaiwa alipata pesa hizo kutokana na kazi yake alipokuwa ameajiriwa katika Mega Shopping Mall.

Abdille na FEL walikana kwamba kati ya Januari 1, 2018 na Septemba 30, 2024 waliiba Sh296,089,084 zake Abdi Mohamed Ali.

Abdille alikana mashtaka 30 na kuomba aachiliwe kwa dhamana akisema “hatatoroka ila atafika kortini wakati wa kusikizwa kwa kesi hiyo.”

Aliongeza kusema ameekeza mali nyingi nchini na hawezi kutoroka aiache.

Upande wa mashtaka haukupinga mshtakiwa akiachiliwa kwa dhamana.

Mahakama ilimwachilia mshtakiwa kwa dhamana ya Sh3 milioni na mdhamini mmoja wa kiasi sawa na hicho.

Pia aliagizwa alipe dhamana ya pesa tasilimu Sh2 milioni afanye kesi akiwa nje.

Kesi itatajwa baada ya wiki mbili kwa maagizo zaidi.