Mkoba wazua kizaazaa katika uwanja wa ndege Mombasa
KULIKUWA na taharuki katika uwanja wa ndege wa Moi, jijini Mombasa jana baada ya mkoba usiokuwa na mwenyewe kupatikana karibu na eneo la maegesho la wageni mashuhuri.
Wataalamu wa bomu walifika kwa wakati uwanjani humo huku juhudi zikiendelezwa za kuwaondoa abiria hadi eneo salama.
Kamanda wa polisi uwanjani humo Evans Mose alisema walichukua hatua kuhakikisha usalama wa abiria na wahudumu wa uwanja wa ndege.
“Tulichukua hatua kuhakikisha hakuna hatari yoyote katika eneo hilo huku tukisubiri maafisa wataalamu wa kutegua mabomu wafike,” akasema Mose.
Alifichua kuwa polisi ambao walikuwa kwenye zamu waligundua mkoba huo kisha wakazingira eneo hilo kutokana na sababu za kiusalama.
“Wataalamu wa bomu walitumia teknolojia kutegua mkoba huo. Kulikuwa na mlipuko mkubwa ambao ulisababisha taharuki lakini tukadhibiti hali,” akasema Bw Mose.
Hakuna majeraha yaliyopatikana wakati wa shughuli hiyo na pia hakuna jengo lolote la uwanja wa ndege ambalo liliharibika.
“Sasa hali imekuwa nzuri na shughuli zinaendelea kama kawaida,” akasema.
Polisi walibaini mkoba hu ulikuwa na vifaa ambavyo vinatumika kwenye karakarana kutoa pumzi kwenye magurudumu ya magari.
Inashukiwa mkoba huo uliangushwa kimakosa na abiria na uchunguzi unaendelea kubaini mmiliki wa mkoba huo.