Mpango wa kukuza viwanda mashinani hatarini kugeuka ‘mradi hewa’, wadau waonya
MRADI wa Sh23.5 bilioni wa Rais William Ruto wa kukuza viwanda katika Kaunti uko hatarini kuwa “mradi hewa”, maseneta wameonya, wakitaja ukosefu wa mipango mizuri na kutoshirikishwa kwa wadau.
Haya yameibuka baada ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Bi Nancy Gathungu, kufichua kuwa ukaguzi wa mradi huu umebaini mapungufu makubwa katika thamani ya fedha.
Gavana wa Siaya, James Orengo amesema kuwa kaunti zilipokezwa mradi huo bila kushauriwa.
Alidai kuwa serikali ya kitaifa iliubuni na kutekeleza mradi huo bila kushirikisha kaunti, na sasa zimeachwa na mabohari ambayo hakuna mwekezaji anayetaka kuyatumia.
“Serikali ya kitaifa haikufanya tathmini ya kutosha iwapo viwanda hivi vinahitajika au jinsi vitakavyosaidia mahitaji ya wenyeji.
Kaunti zilitengwa,” alisema Bw Orengo mbele ya kamati inayoongozwa na Seneta wa Homa Bay Moses Kajwang’.
Alieleza kuwa kaunti zilitarajiwa kuchangia Sh250 milioni kila moja kwa mradi huo, lakini licha ya kuchangia fedha hizo, bado zimekuwa zikipokea mgao mdogo kutoka kwa serikali ya kitaifa.
Kwa mfano, Kaunti ya Siaya imepokea Sh53 milioni pekee kati ya Sh250 milioni ilizoahidiwa, licha ya kuchangia Sh123 milioni.