Habari

Murkomen atangaza Ijumaa kuwa siku ya mapumziko, kuadhimisha Eid-ul-Adha

Na WINNIE ONYANDO Na CHARLES WASONGA June 4th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

WAZIRI wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen ametangaza Ijumaa, Juni 6 kuwa siku ya mapumziko.

Siku hiyo itatoa nafasi kwa Waislamu nchini kufanikisha sherehe za Eid-ul-Adha.

Sikukuu hiyo ambayo husherehekewa kila mwaka baada ya ibada ya Hijja mjini Mecca, huhusisha waumini hao kuchinja mfugo wa miguu minne kwa kumbukumbu ya Nabii Ibrahim aliyekuwa ameagizwa kumchinja mwanawe Ismael.

Dhul Hijja, ambao ni mwezi wa kumi na mbili na wa mwisho katika kalenda ya Kiislamu, huonekana kwa wengi kama nafasi ya kuimarisha imani yao.

Waislamu huadhimisha siku hiyo kwa kuwachinja kondoo au mbuzi kisha nyama hiyo hugawanywa miongoni mwa familia na pia maskini hunufaikia ukarimu huo.

Na inavyoelezwa katika kitabu takatifu cha Quran, Allah alimkabidhi Ibrahim mwana kondoo amtoe kama kafara, dakika chache kabla yake kumtoa kafara.

Sikukuu ya Eid-ul-Adha huja baada ya sherehe za Eid-ul-Fitr, inayoshehekewa baada ya kukamilika kwa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan.

Mwaka huu, Eid-ul-Fitr ilisherehekewa Jumatatu Machi 31, baada ya siku 30 wa mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan ulianza Jumamosi Machi 1,2025.