Mwamko mpya kisiasa
RAIS wa Bunge la Mwananchi, Francis Awino, amezindua vuguvugu la Kenya Moja Coalition analosema linalenga kuwaunganisha Wakenya.
Akizungumza Ijumaa Juni 6, 2025 wakati wa uzinduzi huo, Bw Awino alisema kuwa vuguvugu hilo linalenga kuwaunganisha Wakenya wote bila kujali kabila, rika au eneo wanakotoka.
Kauli mbiu yake ikiwa ni “Maendeleo Bila Ubaguzi”, vuguvugu hilo linalenga kuleta mshikamano wa kitaifa, kurejesha usawa na kuleta maendeleo jumuishi.
“Kenya Moja linalenga kubadilisha historia ya siasa za mgawanyiko, ulafi wa madaraka, na ubaguzi wa kikabila. Kwa kuzingatia hekima ya viongozi wa zamani na kuipa nafasi nguvu mpya za kizazi kipya, harakati hii inalenga kuimarisha ushirikiano wa vijana, wanawake, wanaharakati wa kiraia, na Wakenya wa diaspora,” alisema Bw Awino.
Kulingana na mwanaharakati huyo, Wakenya wengi wanahisi kutengwa na kukosa uwakilishi.
“Hata baada ya katiba mpya ya 2010, changamoto za ufisadi na siasa za kibinafsi zimedumaza maendeleo jumuishi nchini nah ii ndio maana tumezindua vuguvugu hilo,” aliongeza.
Malengo yake ni kuleta mabadiliko ya kiuchumi kwa wote, kupambana na ubaguzi, kuwajibisha serikali na kuwajumuisha vijana katika masuala ya siasa na uongozi.
“Tunapanga mikutano ya mashinani ili kushirikiana na wananchi wote katika kujenga taifa huru na lenye usawa.”