Mwanasiasa mwanamke ahusishwa na ukomboaji lojingi alikoburudika Koimburi -Polisi
MWANASIASA mwanamke Alhamisi alikamatwa na kuhojiwa na maafisa wa upelelezi kuhusiana na madai ya kutekwa nyara kwa Mbunge wa Juja, George Koimburi, tukio ambalo sasa linaonekana kuwa lilipangwa na watu wa karibu naye.
Kwa mujibu wa maelezo kutoka Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI), mwanamke huyo anachunguzwa kwa madai ya kusaidia kupanga utekaji huo ambao imetaja kama wa kuigiza.
Msemaji wa Polisi, Michael Muchiri, alisema kuwa mwanasiasa huyo alihojiwa katika makao makuu ya DCI jijini Nairobi.
“DCI wanahoji mwanamke anayefanana na maelezo haya,” alisema Muchiri.
Jina la mwanasiasa huyo limefichwa kwa sababu za kisheria.
Polisi wanasema simu yake ilitumika kwa muda mrefu Jumapili jioni, siku ambayo mbunge huyo alidaiwa kutekwa nyara.
Aidha, wanaamini kuwa simu hiyo ilitumika kuwasiliana na usimamizi wa hoteli alikokuwa amejificha.
Kwa mujibu wa taarifa ya Mkuu wa DCI, Mohamed Amin, uchunguzi umebaini kuwa Koimburi hakutekwa, bali alilala katika Ellis Bar and Restaurant eneo la Kiganjo, Gatundu.
“Tumeweza kufuatilia mienendo yake yote kuanzia alipoenda kanisani hadi mahali alipolala usiku huo. Hakutekwa bali alijificha,” alisema Amin.
Mbunge huyo alidaiwa kupatikana Jumatatu asubuhi katika shamba la kahawa huko Kiambu, hali ambayo sasa inaonekana ililenga kuonyesha kuwa alikuwa ametekwa nyara na kuteswa.
Kulingana na maelezo kutoka kwa Inspekta Jenerali wa Polisi, Douglas Kanja, Koimburi alibuni tukio hilo ili ahurumie na umma na kuepuka kukamatwa, kufuatia kesi ya ukiukaji wa sheria inayomkabili.
Kufikia Alhamisi, watu watano walikuwa tayari wamekamatwa kwa kuhusishwa na tukio hilo.
Uchunguzi unaendelea huku polisi wakipambana kupata kibali cha kumhoji Mbunge huyo, ambaye bado anapokea matibabu katika Hospitali ya Karen.