Habari

Mwangangi akubali kuongoza mamlaka ya SHA ‘baada ya kufikiria kwa kina’

Na COLLINS OMULO, HELLEN AURA June 4th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Waziri Msaidizi wa Afya Mercy Mwangangi Jumanne alianza kazi rasmi kama Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA), karibu miezi miwili baada ya kuteuliwa kwake.

Saa chache kabla yake kuthibitisha kuwa atachukua wadhifa huo, kulikuwa na ripoti kuwa alikuwa amebadilisha nia. SHA imekuwa ikizongwa na utata, hivyo yeyote anayechukua uongozi wake lazima awe tayari kukabiliwa na darubini kali ya umma.

Hatua hii inajiri wakati ambapo maseneta wanataka wafanyakazi zaidi ya 2,000 wa zamani wa Hazina ya Kitaifa ya Bima ya Afya (NHIF) wafanyiwe uchunguzi mkali ili kuwaondoa wahusika wa uhalifu kabla ya kuhamishiwa rasmi SHA.

Dkt Mwangangi, anayemrithi Robert Ingasira aliyekuwa akiongoza SHA kwa muda, aliahidi enzi mpya ya uwazi katika kusimamia mamlaka hiyo mpya ambayo ni moja ya miradi mikuu ya Rais Ruto.

“Kwa moyo thabiti ninakubali jukumu hili la kuongoza mamlaka hii. Mlisema SHA haina huruma, sasa SHA ina Mercy (huruma),” alisema Dkt Mwangangi.

Aliteuliwa rasmi Aprili 11, 2025 na Waziri wa Afya Aden Duale kuchukua nafasi ya aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu Elijah Wachira, aliyefutwa kazi mwaka jana.

Dkt Mwangangi alisema jukumu lake kuu litakuwa ni kujenga upya imani kwa SHA kupitia uwazi wa kweli katika shughuli zake…

“Tunapaswa kujenga upya imani kupitia uwazi. Tunapaswa kujihusisha na jamii wakati tunasimamia mamlaka hii. Ninachosikia kutoka kwa Wakenya ni kuwa hatujawahusisha vya kutosha,” alisema.

Dkt Mwangangi aliongeza kuwa kuna umuhimu mkubwa wa kuwekeza katika mifumo ya afya ya kijamii kama inavyofanyika ulimwenguni kote, huku asilimia 70 ya Wakenya wakitegemea huduma za afya kutoka kwa zahanati.

Alisema Wakenya wengi kutoka mitaa ya mabanda tayari wamejiunga na mpango wa “Lipa SHA pole pole” uliozinduliwa na serikali.
Rais alipozindua ‘Lipa SHA pole pole’, ilikuwa njia mojawapo ya kuhakikisha Wakenya wanaishi kwa heshima na wanapata huduma za afya. Ni pia kutambua kuwa si kila Mkenya yuko katika daraja moja la ushuru.”

Hata hivyo, maseneta wameonya dhidi ya kuhamisha wafanyakazi wa NHIF moja kwa moja hadi SHA bila kuwachuja.

Kiongozi wa Wengi katika Seneti Aaron Cheruiyot alisema kuwa uchunguzi ni muhimu kuhakikisha waliohusika wa sakata za malipo feki hawapewi nafasi tena ndani ya SHA.

“Lazima kuwepo na mchakato wa uchunguzi. Utekelezaji wake lazima ufanyike kwa njia ambayo hakuna Mkenya anayepata madhara kwa njia isiyo ya haki,” alisema seneta huyo wa Kericho.