Mwili wa mwandishi Ngugi wa Thiong’o wachomwa Amerika
MWILI wa mwandishi maarufu wa vitabu vya fasihi Profesa Ngugi wa Thiong’o ulichomwa nchini Amerika, kwa mujibu wa mwanawe, Profesa Mukoma wa Ngugi.
Profesa Mukoma alisema kuwa hilo lilikuwa takwa la marehemu baba yake. Akizungumza katika mahojiano na Taifa Leo, Mukoma alisema kuwa takwa hilo lilikuwa la “kishujaa”.
“Kwa hivyo, mwili umechomwa, hiyo ndiyo ilikuwa nia yake,” alisema Profesa Mukoma.
“Ninatambua kuwa hilo halilingani na tamaduni zetu za Kenya, lakini kwangu lina mantiki. Micere Mugo naye alichomwa pia.”
Profesa Micere Mugo, gwiji mwingine wa fasihi kutoka Kenya, alifariki dunia nchini Amerika mwaka 2023.
Alishirikiana na Ngugi kuandika tamthilia The Trial of Dedan Kimathi.
Profesa Mukoma aliongeza: “Na kwangu mimi, nafikiri, nikifa, kwa nini nihitaji mwili wangu kama mzigo? Unajua? Kwa nini, sivyo? Kwa hivyo, ndivyo alitaka, na nafikiri tunapaswa kuheshimu na kukubali. Na lazima niseme lilikuwa jambo la kishujaa sana kwake na pia lenye maono.”
Profesa Ngugi alifariki Mei 28 akiwa na umri wa miaka 87 katika jiji la Atlanta, Amerika.